UHUSIANO ULIOPO KATI YA IMANI NA SADAKA UNAYOITOA MBELE ZA MUNGU

 

Ni muhimu sana ukijua ya kwamba upo uhusiano kati sadaka uliyoikusudia kuitoa mbele za Mungu na imani yako kwa Mungu huyo unayemtolea hiyo sadaka.

Sadaka ni kama kibebeo mfano bakuli, kama ukipeleka sadaka yako ambayo ni kibebeo mbele za Mungu halafu haina imani ni sawa na umepeleka kibebeo kitupu.

Kwa sababu Mungu anaangalia kwanza imani kabla ya kuangalia sadaka uliyoitoa.

Waebrania 11 : 4

“Kwa imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo ijapokuwa amekufa angali akinena”

Angalia yale maneno “kwa imani”, halafu tuangalie mambo yafuatayo:

i.                    Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo- Ebrania 11 : 1

Kama Habili alitoa sadaka kwa imani basi kuna kitu alikuwa anakitarajia akipate kutoka kwa Bwana wakati anatoa sadaka yake.

ii.                  Chanzo cha imani ni kusikia neno la Kristo – Warumi 10 : 17

Na kama chanzo cha imani ni kusikia neno la Kristo, basi ujue pia Habili kuna namna alisikia sauti ya Mungu ndani yake ikimuagiza atoe sadaka.

Biblia haijatuambia walipata wapi agizo la kutoa sadaka wakati ule, lakini wakati ule tunaona wote wawili wanakwenda kumtolea Mungu sadaka zao. Na mmoja anapata kibali yeye na sadaka yake bali mwingine hapati kibali yeye na sadaka yake

Mwanzo 4 : 3 – 7

Sadaka ya Habili ilikuwa imebeba imani ndani yake ndio maana ilipofika mbele za Mungu aliifurahia lakini sadaka ya Kaini haikuwa imebeba imani ndani yake. Kumbuka kuwa pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu. – Ebrania 11 : 6

Kwa hiyo tofauti ya sadaka iliyotolewa na Habili na Kaini ilikuwa kwenye imani.

-          Na ni hatari sana kutoa sadaka bila imani, kwa sababu imani ndio inayokupa kibali kwa Mungu na sio sadaka.

-          Watu wengi wanadhani watakubaliwa na Mungu kwa sababu wanatoa sana sadaka. Na kwa sababu hiyo wanatoa kwa mazoea na kwa kufuata mkumbo tu.

-          Sadaka yoyote haitolewi kwa mazoea wala kwa mkumbo bali sadaka inatolewa kwa imani.

Imani ndio inayounganisha sadaka yako na moyo wako mbele za Mungu.

-          Mungu akiingalia sadaka iliyobeba imani ndani ake anauona moyo wako, kwa sababu ndani ya imani kuna tarajio, na hilo tarajio ndio haja ya moyo wako.

Unapotoa sadaka mbele za Mungu pasipokuwa na imani ni sawa na hauamini kuwa Yeye yupo na pia hauamini kuwa anaweza akaleta matokeo ya sadaka uliyotoa, ndio maana anakuwa haifurahii hiyo sadaka. Kumbuka pasipo imani haiwezekani kumpendeza Mungu na kila amwendeaye Mungu ni lazima aamini kuwa yeye yupo.

Ukiangalia ule mstari wa Mwanzo 4 : 3 – 7 unaona ya kuwa Kaini alikosa kibali kutoka kwa Bwana sio kwa sababu ya kutokutoa sadaka bali ni kwa sababu alitoa sadaka pasipokuwa na imani.

-          Ule mstari wa 7 unasema “kama ukitenda vyema hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko…”

-          Tafsiri yake ni kwamba Mungu alikuwa anamwambia Kaini kuwa jambo lolote linalofanyika pasipo imani halimpendezi Mungu maana yake linakuwa ni dhambi.- Warumi 14 : 23b

-          Hii inaonyesha kuwa Kaini hakutenda vyema bali alitenda dhambi kwa kutoa sadaka bila imani ndio maana Mungu akamwambia kuwa kama ukitenda vyema hutapata kibali?

-          Macho ya Mungu kabla hayajaitazama adaka uliyoitoa yanatazama kwanza kilichobebwa ndani ya hiyo sadaka. Kwa hiyo kama sadaka yako haina imani basi Mungu anakuhesabia kuwa hujafanya jambo jema. Maana yake hapendezewi na hiyo sadaka yako. Hivyo hawezi akaikubali.

Sadaka pasipo kuwa na imani ni sawa na kuandika barua isiyokuwa na address kwa hiyo haijulikani inakwenda kwa Mungu yupi, hivyo usitegemee kupata majibu.

Sadaka inaweza ikabadili mfumo wa maisha yako (maisha yako yanaweza yakawa mazuri au yakawa mabaya).

-          Unaweza ukapokea baraka au laana unapotoa sadaka

Ø  Wapo waliotoa sadaka wakakataliwa na kupata laana:

Mfano 1: Mfalme Sauli

1 Samweli 15 : 22 – 23

-          Sauli aliambiwa na Mungu akawaangamize Waamaleki wote na mali zao lakini yeye alikwenda akaua watu na akabakisha mifugo iliyonona ili aje aitoe sadaka kwa Mungu.

-          Mungu akaikataa sadaka yake kwa sababu hakuitii sauti yake iliyomwagiza.

 

Mfano 2: Anania na Safira

Matendo 5 : 1 – 11

-          Huyu mtu na mkewe walipatana wakauza kiwanja chao ili waje walete fedha hiyo kama sadaka kwa Mungu, lakini walizuia kwa siri baadhi ya kiasi cha fedha katika ile thamani waliyoiuza na wakadanganya kuwa wamekiuza kwa fedha pungufu.

-          Mungu aliamua kuwaua mbele ya kapu la sadaka kwa sababu walikuwa ni waongo; waliamua kuitii sauti ya Shetani iliyowashawishi wazuie kwa siri kiasi fulani cha fedha badala ya kuitii sauti Mungu iliyowaagiza wakauze kiwanja na kuileta thamani yote ya fedha mbele za Mungu

-          Kumbuka unaweza ukawa na imani lakini isiyo ya Kristo. Imani ya Kristo huwa inakuja na Neno la Kristo ndani yake, na imani ya shetani huwa inakuja na neno la shetani ndani yake. Ndio maana mtume Petro aliwaambia ni kwa nini shetani amewajaza kumwambia uongo Roho Mtakatifu.

 

Ø  Pia wapo waliobarikiwa baada ya kutoa sadaka

Mfano 1: Ibrahimu

Mwanzo 22 : 1 – 12 – 14

-          Ibrahimu alipoambiwa amtoe mwanawe kuwa sadaka kwa Mungu, wala hakumzuia bali alikubali kumtoa.

-          Ndipo Mungu alipoahidi kumbariki Ibrahimu na kumfanya kuwa baraka kwa mataifa yote.

-          Ibrahimu aliamua kuitii sauti ya Mungu bila kujali mazingira aliyokuwa nayo, kwa sababu Isaka ndiye mtoto wa pekee wa ahadi aliyekuwa naye. Kwa kawaida ilikuwa ni vigumu lakini alitii.

 

Mfano 2: Mfalme Sulemani

2 Nyakati 1 : 6 – 13 & 1 Wafalme 3 : 4 – 5

-          Mfalme Sulemani alipopakwa mafuta kuwa mfalme aliamua kumtolea Mungu sadaka.

-          Hiyo sadaka ilimfanya Mungu ashuke azungumze naye kwenye ndoto ili ampe haja ya moyo wake.

-          Hatukuambiwa kuwa alitoa sadaka ya shukrani au alitoa sadaka ya namna gani lakini tunajua kuwa Mungu alijibu.

Hii inaonyesha yakuwa tunapotoa sadaka yoyote Mungu huwa anaifuatilia. Hivyo kila sadaka unayoitoa huwa ina matokeo yake. –  1 Wakorintho 9 : 6

NB: Hii inatupa kuwa makini sana tunapotoa sadaka mbele za Mungu tusije tukajitwalia laana badala ya baraka.

KAZI YA IMANI NDANI YAKO UNAPOTOA SADAKA

Ni vizuri kwanza ukajua kuwa kuna aina mbalimbali za sadaka ambazo mtu anaweza akazitoa mbele za Mungu

-          Unaweza ukatoa sadaka ya fedha, au mali, au hali, au ukatoa nguvu zako, au ukatoa mwili wako kutumika na ikahesabika kuwa ni sadaka mbele za Mungu, au pia unaweza ukatoa sadaka ya ukarimu n.k

Warumi 12 : 1

-          Sadaka yoyote ile ni lazima ibebe imani ndani yake ndipo itakapompendeza Mungu

 

a.     Unapata kuwa na amani juu ya kazi uliyopewa na Mungu uifanye hata kama mazingira uliyopo hayakuruhusu ufanye hivyo

Kuna wakati Mungu anaweza akakusemesha utoe sadaka ambayo kiuhalisia ni vigumu sana kuitoa kutokana na mazingira uliyopo, lakini imani ndani yako inawahi kukamata moyo wako ili uwe na amani juu ya hicho ulichoamriwa na Mungu ukifanye.

Waebrania 11 : 31

Yoshua 2 : 1 – 8 – 10

Biblia inasema kuwa Rahabu Yule kahaba aliwasaidia wale wapelelezi wa Israeli kwa imani. Hii ni kwamba kuna namna ambayo Mungu alizungumza na Rahabu juu ya kuwahifadhi wale wapelelezi hata kama kwa uhalisia walikuwa ni maadui zao. Ile sauti ya Mungu ndani ya moyo wa Rahabu ikatengeneza imani. Nayo imani ikaachilia amani ndani ya moyo wa Rahabu ili asiogope kuwakaribisha wale wapelelezi.

-          Usidhani ilikuwa ni kitu chepesi kwa Rahabu kuwakaribisha na kuwahifadhi wale wapelelezi, haikuwa kitu kirahisi. Ndio maana ilibidi Mungu aachilie amani ndani yake ili kazi aliyopewa ifanyike.

-          Rahabu alikuwa anajua kabisa kuwa hawa watu wanakuja kuangamiza mji wao wote lakini bado alipata amani ya kuwapokea na kuwahifadhi wasiuawe na majeshi ya mji wa Yeriko.

-          Imani huwa inaachilia amani ndani ya mtu – Warumi 5 : 1

-          Hivyo hakuna amani pasipo kuwa na Imani.

-          Sadaka aliyoitoa Rahabu ilikuwa ni sadaka ya utu au ufadhili.

Na kwa sababu hiyo, Rahabu kwa njia ya imani amepata heshima kubwa kuliko hata wale wapelelezi

-          Biblia inatambua jina la Rahabu lakini majina ya wale wapelelzi hatujajulishwa.

-          Pia Rahabu anatajwa kwenye ukoo wa Yesu kitu ambacho si kila mtu alipata kuwa na heshima hiyo.

 

b.     Imani inampa Mungu nafasi ya kushughulikia maisha yako ya baadae au msimu mpya kwenye maisha yako.

Kuna watu ambao huwa wanasikia ndani yao msukumo wa kutoa sadaka kila wanapokaribia kuingia katika msimu mpya kwenye maisha yao.

-          Sasa usidhani tu kuwa ni jambo la kawaida bali ni sauti ya Mungu inazungumza ndani yako kwa sababu Mungu anataka ashughulikie hali au mazingira unayoyaendea kwenye hatua nyingine ya maisha yako.

Mfano 1: Waebrania 11 : 7 & Mwanzo 8 : 15 – 21

Hizi ni habari za Nuhu wakati anatoka kwenye safina baada ya maji kupungua juu ya nchi wakati wa Gharika.

-          Biblia haijatuonyesha kama kuna sehemu Mungu alimwambia Nuhu amtolee sadaka bali Nuhu mwenyewe alijua umuhimu wa Mungu kuhusika kwenye msimu mpya wa maisha yao kwa sababu dunia nzima walikuwa wamebaki watu nane tu, pamoja na hao wanyama na ndege waliokuwa nao kwenye safina.

-          Kumbuka kuwa baada ya gharika, kila kitu juu ya uso wa dunia yote kiliharibika. Lakini sadaka aliyoitoa Nuhu ilifanya mambo yafuatayo:

i.                    Ilimfanya Mungu aahidi kutoipiga tena dunia kwa maji,

ii.                  Pia alirejesha majira na vipindi vya hali ya hewa vilivyoharibiwa na maji.

Kwa hiyo kwa kupitia sadaka aliyoitoa Nuhu, Mungu alishughulikia maisha ya wale watu nane baada ya kutoka kwenye safina.

Mfano 2: habari za Mfalme Sulemani alitoa sadaka mbele za Mungu ili Mungu ashughulike na msimu mpya kwenye maisha yake ya yeye kuwa mfalme wa Israel

1 Wafalme 3 : 4 – 5

 

 

 

c.      Imani inaleta ushirika kati ya mtoa sadaka na Mungu anayetolewa hiyo sadaka

Unapotoa sadaka kwa Mungu wako ni ishara mojawapo ya kuwa kuna ushirika kati yako na Mungu wako.

-          Kwa sababu sadaka inajulisha ni Mungu yupi unayemtumikia

-          Kama unatambika basi utatoa sadaka kwa mizimu unayoitambikia lakini kama unamtumikia Yehova Mungu wa kweli aliye hai basi utatoa sadaka kwake.

-          Sasa kinachokuunganisha wewe na Mungu unayemtolea hiyo sadaka sio sadaka bali ni imani. Kwa sababu ili utoe sadaka kwa Mungu aliye hai, ni lazima kuwa ulisikia na kuitii sauti ya Kristo ndani yako ikajenga imani ya Kristo moyoni mwako ndio maana ukaenda kumtolea Mungu sadaka; lakini kama ulisikia sauti ya shetani ndani yako ikajenga imani ya kishetani moyoni mwako basi utakwenda kutoa sadaka kwa miungu na mizimu.

-          Imani ndio inayokusukuma ni wapi pa kuipeleka sadaka yako.

Na ni muhimu kukumbuka ya kuwa mahali ilipo hazina yako ndipo na moyo wako utakapokuwepo. Mathayo 6 : 21

-          Imani huwa inakamata usikivu wa mtu ili kutii sauti ya Mungu anayemtumikia.

-          Kama huwa unatoa sadaka kwa miungu basi hiyo miungu inakamata moyo wako ili usisikie sauti nyingine bali sauti ya hiyo miungu tu.

No comments:

Post a Comment

Katika maisha yako usisikilize watu wanasema nini bali msikilize Mungu anasema nini, kwa sababu watu hawajui ni nini ambacho Mungu amekupang...