SIRI YA MSALABA WA YESU KRISTO

Lengo la somo hili ni kukusaidia kujua siri iliyoko kwenye msalaba wa Yesu Kristo na thamani yake kwetu.

1 Wakoritho 1 : 17, 18 – Maana Kristo hakunituma ili nibatize, bali niihubiri habari njema; wala si kwa hekima ya maneno, msalaba wa Kristo usije ukabatilika. Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.

Thamani ya kitu chochote inapimwa kwa gharama iliyotumika kukipata hicho kitu. Kama gharama ya kitu ni ndogo basi na thamani yake ni ndogo; na kama gharama yake ni kubwa basi hata na thamani yake ni kubwa pia.

Kwa mfano thamani ya watoto ulionao inaweza kutofautiana kutokana na jinsi ulivyowapata. Yule aliyepata watoto kwa taabu ataona watoto hao wanathamani kubwa sana kuliko Yule aliyepata watoto kwa wepesi, hivyo ikakupelekea kumpenda zaidi Yule uliyempata kwa taabu zaidi kuliko Yule ulimpata kwa urahisi.

Pia ni sawa na thamani ya madini au vito vya thamani. Dhahabu haiwezi ikawa sawa na shaba kwa sababu upatikanaji wa dhahabu ni tofauti na upatikanaji wa shaba. Shaba inapatikana kwa wepesi zaidi kuliko dhahabu.

Hivyo ndivyo ilivyo thamani ya wokovu wetu, kwa sababu wokovu wetu haukupatikana kirahisi bali ilimbidi Yesu Kristo aache enzi yake na utukufu wake aliokuwa nao kule mbinguni ili aje afe kifo cha msalaba kwa ajili ya kutuokoa sisi wanadamu.

Wafilipi 2 : 5 – 8 – Hakuona kule kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kushikamana nacho, bali akajifanya hana utukufu, akajinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba.

Waebrania 12 : 2 – Ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu

-          Kwa tafsiri nyingine ni kwamba Yesu aliona kuwa kuendelea kuwa na utukufu na heshima yake huko mbinguni hakumfai kitu chochote wakati kazi yake huku duniani inaendelea kuharibika.

-          Kwa hiyo alithaminisha ukombozi wetu na utukufu wake huko mbinguni akaona ni bora aache enzi na utukufu ili aje duniani kutuokoa wanadamu tutoke kwenye mikono ya adui Shetani.

-          Haikuwa rahisi kwake lakini kwa sababu aliona thamani kubwa ya kutuokoa basi ikambidi aje kufa msalabani kwa ajili yetu.

-          Kifo cha msalabani kilikuwa ni kifo cha aibu kubwa sana na cha kudharaulika sana

Usiutazame msalaba kama mbao mbili zilizounganishwa pamoja bali utazame msalaba kama ishara ya thamani ya ukombozi wako katika Kristo Yesu.

Sio kila msalaba unaouona ni msalaba wa Kristo, kwa sababu Yesu hakusulibiwa peke yake, kulikuwa na watu wengine ambao hao walikuwa ni wanyang’anyi. Na wote walikuwa wamesulibiwa msalabani

-          Kwa hiyo usitishike utakapomuona mtu amebeba au amevaa msalaba

-          Na hata kuhubiri injili, Biblia inatuambia tuhubiri injili ya Yesu aliyesulibiwa. Hii inamaanisha kuwa kuna watu wanaweza wakahubiri habari za miujiza na kufanikiwa lakini vyote hivyo visitokane na msalaba yaani wokovu.

-          Unaweza ukafanikiwa ndani ya wokovu na pia ukafanikiwa nje ya wokovu

-          Unaweza ukapokea uponyaji ukiwa ndani ya wokovu au ukaponywa ukiwa nje ya wokovu. Kwa hiyo uwe makini na injili unayoletewa.

Biblia inatuambia kwamba neno la msalaba kwa wanaopotea ni upuzi bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu.

-          Maana ya neno la msalaba ni; ujumbe wa msalaba, au kilichobebwa kwenye msalaba, au thamani ya msalaba, au siri iliyoko kwenye msalaba, au kazi iliyofanyika msalabani n.k

-          Kwa lugha nyingine ni kwamba Mungu anataka tuone msalaba kuwa ni jambo la thamani sana kwetu japokuwa watu wengine wasiojua thamani hiyo wanapuuzia.

NB: Sasa tambua kuwa kutokujua thamani ya jambo fulani haibadilishi uthamani wa jambo hilo. Kama wewe ni wa thamani, na sisi hatujui thamani yako, basi haitabadilisha thamani uliyonayo bali sisi ndio ambao hatutafaidika na thamni hiyo uliyonayo.

-          Hivyo usipojua thamani ya msalaba haitabadilisha thamani yake bali wewe ndio hautafaidika na thamani hiyo ya msalaba.

NB: Natamani pia ujue kuwa kazi ya Yesu hapa duniani isingekuwa na maana yoyote kama asingepitia msalabani. Kwa sababu wako manabii waliotenda miujiza ambayo ilikaribiana na aliyoitenda Yesu, wapo waliofufua wafu, wapo walioponya watu, wapo waliofanya ishara kubwa na za ajabu zinazokaribiana na alizofanya Yesu, lakini utofauti wa Yesu na hao manabii au mitume ulikuwa ni kwenye kazi ya msalaba. Ni muhimu sana ukafahamu jambo hilo.

-          Yesu asingekufa msalabani basi tungemfananisha na manabii au mitume wengine.

-          Kwa hiyo msalaba ndio unaomtambulisha Yesu ni nani, na ndio unaomtofautisha Yesu na watumishi wengine.

-          Injili yetu sio ya Yesu wa kabla ya msalaba bali injili yetu ni ya Yesu aliyesulibiwa msalabani, akafa na akafufuka.

BAADHI YA MABADILIKO YALIYOTOKEA KATIKA ULIMWENGU WA ROHO WAKATI DHAMBI ILIPOINGIA ULIMWENGUNI

Inawezekana ukawa unajiuliza ni kwa nini Yesu alikufa msalabani? Lakini kabla ya kuendelea mbali zaidi ni vizuri kwanza tukaona mambo yaliyotokea pale katika bustani ya Edeni wakati Adamu na Hawa walipomuasi Mungu kwa kutoyatii maagizo waliyopewa na Mungu. Baada ya hapo ndipo utakapojua ni nini msalaba umekuja kufanya.

Na baadhi ya mambo hayo ni:

i.                   Mwanadamu alipoteza nafasi ya kiutawala aliyopewa na Mungu alipoumbwa

Mwanzo 3 : 9 – Mungu akamwita Adam akamwambia uko wapi?

Lile neno “uko wapi” haimaanishi kuwa Mungu hakuwa anamuona Adamu kama mtu bali hakuwa anamuona Adamu kama mtawala wa hii dunia. Hakumuona kwenye nafasi yake.

Kazi ya dhambi ni kuharibu uhusiano wako na Mungu kwanza kabla ya kuleta athari za kimwili.

-          Ndio maana wale wanaofanya dhambi kwa kujifichaficha wanadhani wako salama kumbe walishapoteza mahusiano yao na Mungu kitambo tu.

Kabla dhambi haijaingia ulimwenguni, sisi ndio tuliokuwa wakuu wa dunia hii. Ndio maana Mungu alimwambia Adamu na Hawa kuwa waende wakaitawale dunia, wakatawale samaki wa baharini, ndege wa angani na kila kinachotambaa juu ya ardhi.

Mwanzo 1 : 26, 28 – Mzae mkaongezeke ili mkatawale ndege wa angani, samaki wa baharini, na wanyama na nchi yote pia.

-          Hiyo ilikuwa ni nafasi ya kiutawala na kiumiliki tuliyokuwa nayo juu ya ulimwengu huu.

-          Dunia haikupaswa kututawala sisi bali sisi ndio tulipaswa tuitawale dunia.

-          Na pia tulikuwa tumepewa utiisho na mamlaka ya kuiamuru dunia nayo ikatusikiliza.

-          Kuna mambo kwenye maisha haya tunayoishi sasa hatukutakiwa kuhangaika kabisa kwa sababu yanahitaji uyaamuru ili yatokee lakini kwa sababu nafasi ya kiutawala hauna basi huwezi ukayaamuru ili yatokee, hivyo utabaki unahangaika.

Zaburi 8 : 4 – 8 – Umemtawaza juu ya kazi za mikono yako, umevitia vitu vyote chini ya miguu yake…

Zaburi 82 : 6 – 7 – Mimi nimesema ninyi miungu, na wana wa Aliye juu…

-          Mwanadamu ndiye aliyeumbwa awe mungu wa dunia hii na sio shetani, lakini kwa sababu mwanadamu huyo alitenda dhambi ikapelekea kupoteza ile nafasi ya kuwa mungu au mtawala katika hii dunia.

-          Tulivyopoteza nafasi hiyo ndipo shetani akaichukua yeye hiyo nafasi, akawa ndiye mungu wa dunia hii.

2 Wakorintho 4 : 4 – mungu wa dunia hii ni shetani.

 

ii.                 Tulipoteza uwepo wa Mungu ndani yetu ambayo tafsiri yake ni kufa/mauti

Mungu aliwaambia Adam na Hawa ya kuwa wakila tunda la mti wa ujuzi wa mema na mabaya hakika watakufa. Mwa 2 : 16 - 17

-          Mauti aliyoiongelea Mungu hapa ilikuwa ni mauti ya kiroho yaani kupoteza Uwepo wa Mungu kwenye maisha yao. Ni bora ukafa kifo cha kimwili lakini sio kifo cha kiroho.

-          Kifo cha kimwili ni pale ambapo roho ya mtu inatengana na mwili wake bali kifo cha kiroho ni pale ambapo mwanadamu anapoteza uwepo wa Mungu ndani yake. Ndio maana watu ambao hawajaokoka wanaitwa wafu japo bado wanaishi duniani.

NB: Uwepo wa Mungu ndio uzima ndani ya roho ya mtu, kama hauna Uwepo wa Mungu ndani yako maana yake roho yako haina uzima. Hicho ndicho kifo cha kiroho.  Yohana 17 : 3 & 1Yohana 5 : 11 - 12

Huwezi ukamjua Mungu usiyemtumikia, na Mungu unayemtumikia ndiye unayemjua. Maana yake kuna kuwa na ushirika kati yako na Mungu.

-          Dhambi inakutenga mbali na uwepo wa Mungu, kwa sababu Mungu hachangamani na dhambi.

-          Kwa hiyo unatakiwa ujue kuwa unaporuhusu dhambi kutawala maisha yako basi ujue ni tayari ulishakufa kiroho kwa kuwa uwepo wa Mungu ulikwisha ondoka ndani yako.

1 Wakorintho 15 : 22

-          Mauti ilipata mlango wa kuingilia duniani kwa njia ya Adamu, lakini uzima uliletwa na Yesu Kristo

2 Wakorintho 5 : 14 – 15 – Yesu alikufa kwa ajili ya wote

Kwa sababu Yesu Kristo ni lango, hivyo kifo chake kiliwakilisha vifo vya watu wote, ili sisi tusife tena bali tuwe hai kwa sababu kuna aliyekufa kwa niaba yetu.

-          Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Adam ambaye naye alikuwa ni lango ndio maana alipotenda dhambi yeye tulihesabiwa wote tumetenda dhambi.

Uwepo wa Mungu unapoondoka ndani yako unapoteza ushirika na Mungu. Kwa hiyo unakosa kuwa na mawasiliano na Mungu.

 

iii.               Kuanza kwa kipindi cha utawala wa laana juu ya maisha ya mwanadamu

Kabla ya dhambi kuingia ulimwenguni hakukuwa na laana. Laana imekuja kama adhabu kutokana na dhambi kuingia duniani.

Mwanzo 3 : 14 – 19 – Mungu anatoa laana kwa nyoka, kwa mwanaume, kwa mwanamke na kwa ardhi

Swali: Ulishawahi kujiuliza kwa nini ardhi ilaaniwe wakati aliyetenda kosa ni mtu?

Jibu ni kwamba: mtu ndiye aliyewekwa kuwa mwangalizi wa kila kilichopo duniani, kwa hiyo kosa lake linaathiri mpaka vile vilivyowekwa chini yake ikiwemo ardhi. Hiyo ndiyo sheria iliyopo kwenye ulimwengu wa kiroho. Ndio maana kwa wakati ule ilikuwa kama baba ndiye amefanya kosa linalompasa kuuawa basi hafi peke yake bali hata familia yake, na mifugo yake na vitu vyake vyote vinateketezwa, pia watu wanachukuliwa na kuuawa au wanakuwa watumwa. Mfano:  Yoshua 7 : 1 - 26

-          Tafsiri ya karibu ya laana ni kutofikia uwezo wa nguvu zako. Yaani unazalisha kingi lakini unachopata ni kidogo.

-          Unaweza ukawa unafanya kazi ya kuajiriwa na unapata mshahara mzuri tu lakini maisha yako hayafanani na hela unayopata. Au unaweza ukawa unajuhudi na bidii katika kufanya biashara zako na ukafanikiwa kupata kipato kizuri lakini fedha hizo zinaishia kutibu magonjwa, kulipa madeni, misiba n.k na wala zisikusaidie kujenga na kuendeleza maisha yako. Hiyo inaitwa laana.

-          Kuna mambo unaweza ukayaona ni ya kawaida kwenye maisha yako lakini kumbe unatembea chini ya laana.

Ø  Nyoka hakuumbwa ili atembee kwa tumbo na kula mavumbi ya nchi bali laana ilimfanya awe hivyo alivyo sasa; mwanamke hakuumbwa ili azae kwa uchungu mwingi bali laana ndio imemfanya awe hivyo;  wala mwanaume hakuumbwa ili ale kwa kuteseka kiasi hicho bali laana ndio imemfanya awe hivyo alivyo. Kwa hiyo vyote hivyo inaonyesha jinsi laana ilivyobadilisha mfumo wa maisha ya mtu.

Ø  Ni muhimu ukajua kutofautisha kati ya kutembea katika laana na kutembea katika mapenzi ya Mungu. Laana sio mapenzi ya Mungu bali ni adhabu kutoka kwa Mungu iliyotokana na kuasi kwa mwanadamu.

Ø  Maisha ya laana ni maisha ya chini ya kiwango. Mtu unaishi chini ya uwezo uliopewa na Mungu

Yako mambo mengi ambayo yaliharibika kipindi dhambi inaingia ulimwenguni lakini leo tumejifunza hayo machache.

KAZI YA MSALABA

Tunapoangalia kazi ya msalaba tunapata kujua sababu zilizomfanya Bwana Yesu Kristo apite kwenye njia hii ya msalaba kwa ajili ya kutupatia ukombozi wetu.

a.     Kuleta ukombozi wa mwanadamu kwa kupitia damu ya thamani ya Yesu Kristo

Yesu Kristo alikufa msalabani kwa ajili ya dhambi zetu ili tusamehewe dhambi zetu na kuwa watoto wa Mungu aliye juu. Na ukumbuke kuwa dhambi ilikata mawasiliano kati ya Mungu na Mwanadamu, kwa sababu mwanadamu alikuwa chini ya utawala wa shetani hivyo ilibidi akombolewe kutoka huko kwenye ufalme wa giza.

Yohana 3 : 16, - 18 – Mungu alitupenda, akamtoa Mwana wake wa pekee ili afe kwa ajili yetu

Isaya 53 : 5 – na kwa kupigwa kwake sisi tumepona

Waefeso 1 : 7 & Wakolosai 1 : 13 - 14 – Ukombozi ni sawa sawa na msamaha wa dhambi

-          Kwa kupitia msalaba tumepokea msamaha wa dhambi ambao ndio ukombozi wetu.

-          Kazi kubwa moja wapo ya Yesu Kristo kuja duniani ni kwa ajili ya kutuokoa kutoka kwenye nguvu za giza na kutuingiza kwenye ufalme wake.

-          Na kwa sababu tulikuwa tumemkosea Mungu ilibidi kwanza tupokee msamaha wa dhambi zetu ndipo tubadilishwe na kuwa watoto wa Mungu.

-          Damu ya Yesu iliyomwagika pale msalabani ilitosha kabisa kutufutia makosa yetu yote mbele za Mungu na tukawa wapya kana kwamba ni kama hatujawahi kutenda dhambi kabisa.

Tulipotenda dhambi, katika ulimwengu wa roho ni sawa na tuliuzwa kwa shetani, kwa hiyo ilibidi Yesu Kristo atununue. Na kitu pekee cha thamani kilichotoshea kulipa thamani yetu ilikuwa ni damu yake pekee ambayo ni damu ya Mungu Baba. – Ufunuo 5 : 9

-          Katika Agano la Kale walitumia damu za wanyama katika kufunika makosa lakini hazikutosha kufuta makosa ya mwanadamu, kwa hiyo ilibidi ipatikane damu iliyo bora zaidi ili ifute makosa ya mwanadamu.

-          Hapo ndipo utakapojua ni kwa nini ilimbidi Yesu aje duniani katika umbo la mwanadamu na auvae mwili wa kibinadamu. Roho haina damu kama mwili ulivyo na damu. Kwa hiyo ilibidi avae mwili wa kibinadamu lakini asichangamane damu yake na mwanadamu. Ndio maana alizaliwa kwa uweza wa Roho mtakatifu. Kilichotafutwa hapo ilikuwa ni tumbo la Bikira Mariam ili kumleta Yesu duniani na sio Yusufu.

-          Hakukuwa na namna yoyote ya Yesu kutuokoa akiwa yuko mbinguni, ilimbidi aje duniani ndipo atuokoe.

Hivyo tunapouangalia msalaba wa Yesu Kristo tunaona ukombozi wetu pale.

 

b.     Kushughulikia roho ya mauti iliyokuwa inatawala juu ya mwanadamu

Msalaba ulihusika kuleta uzima ndani ya mtu kutoka kwenye hali ya mauti aliyokuwa nayo mtu wakati angalipo kwenye maisha ya dhambi

Waebrania 2 : 14 – 15

Mauti ilipata nguvu juu ya mwanadamu kwa sababu ya dhambi alizozitenda. Na ndio maana mshahara wa dhambi ni mauti, kwa kuwa mauti ni matokeo ya dhambi.  Warumi 6 : 23

-          Na lango hili la mauti lilifunguliwa kwa Adamu, hivyo mauti ikawapata wanadamu wote

-          Kwa sababu hiyo ilimpasa Yesu kama lango, kufa kwa ajili na kwa niaba ya kila mtu ili kwa kupitia yeye kila mtu awe na uzima. – 1 Wathesalonike 5 : 9 - 10

-          Hivyo Yesu aliihukumu roho ya mauti kwa njia ya mauti yake pale msalabani.

-          Yesu alitumia mauti kuhukumu mauti. Ni kama vile ambavyo unaweza ukahukumu sadaka zilizotolewa kwa miungu kwa njia ya kuachilia sadaka yako mbele za Mungu ili kuhukumu sadaka hizo.

Warumi 6 : 10 – Maana kwa kule kufa kwake aliifia dhambi mara moja tu, lakini kwa kule kuishi kwake amwishia Mungu.

Kwa kupitia msalaba wa Yesu tumerejeshewa uzima ambao ni uwepo wa Mungu ndani yetu, kwa kuwa Yesu Kristo ndiye uzima wetu na anakaa ndani yetu.

 

 

c.      Kufuta sheria za kimwili zilizokuwa zinatawala mioyo yetu kinyume na mapenzi ya Mungu

Kazi nyingine ya msalaba ilikuwa ni kufuta hati ya mashitaka na sheria za kimwili ambazo zilitawala ndani ya mioyo ya watu.

Wakolosai 2 : 13 – 16

-          Na kwa kupitia hizo sheria, watu walikuwa wakipingana na mapenzi ya Mungu, hivyo walikuwa wanafuata mapokeo yao.

-          Kuna mambo ambayo kiuhalisia yaliletwa na torati ya Musa lakini ilikuwa ni kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Na Yesu Kristo alipokuja ulimwenguni aliyarekebisha hayo mambo ili tusiishi tena kwa sheria bali kwa Neno lake.

-          Na watu walikuwa wameziweka moyoni hizo sheria na mapokeo hayo kuliko kuweka  Neno la Mungu mioyoni mwao. Kwa hiyo ndani ya mioyo yao kulijaa torati lakini haikuwasaidia kumfahamu Mungu kama Mungu mwenyewe alivyotaka.

Mfano: Mtume Petro alikataa kwenda kuchangamana na wamataifa kwa sababu aliwaona ni najisi kwa kuwa hawakuwa Wayahudi (kipindi kile ilikuwa Wayahudi hawachangamani na watu wa mataifa mengine, hata kula nao pamoja ilikuwa hairuhusiwi). Lakini Mungu alimshurutisha aende kwao kuwahubiria habari ya wokovu ulio ndani ya Yesu Kristo.  Matendo 10 : 1 – 34 – 48.

Wako watu duniani mpaka leo wanashindwa kumpokea Yesu Kristo katika maisha yao kwa sababu ya mapokeo ya dini zao na sheria zilizopo kwenye torati, na nyingine ni sheria zinazotokana na jamii walizopo.

 

d.     Kuleta  utu mpya ndani ya kila mtu atakyempokea Kristo ili asitumikie dhambi tena

Kazi nyingine ya msalaba ilikuwa ni kushughulikia mabadiliko ya mtu wa ndani ili maisha yetu ya kimwili yabadilike. Hali yetu ya kimwili inategemea sana hali yetu ya kiroho. Kama mtu wa ndani hajabadilika na unasema umeokoka basi kiuhalisia bado hujaokoka.

Kuokoka ni kubadilika. Kubadilika mtazamo wako, mwenendo wako, n.k. Utu wako wa ndani unafanywa upya. – Waefeso 4 : 22 - 24

Warumi 6 : 5 – 6

Yesu Kristo anapotusamehe dhambi zetu hatuachi tu tukajiongoza wenyewe bali pia anashugulika na kubadilisha utu wetu wa ndani ili tusiwe tena watumwa wa dhambi bali tumtumikie Yeye peke yake.

Kwa hiyo mabadiliko ya mtu wa ndani sio jitihada zako bali ni kazi aliyoifanya Bwana Yesu pale msalabani. Kwa maneno mengine ni kwamba kufa kwa Yesu pale msalabani sio tu kwa ajili ya kukuokoa peke yake bali pia na kuubadilisha utu wako wa ndani.

-          Ile kwamba unakataa dhambi sio kwamba ni ujanja wako bali ni kazi ya msalaba. Kwa hiyo usijisifu, bali mtukuze Mungu.

-          Kwa maneno mengine ni kwamba Yesu alituzaa kwa upya pale msalabani.

-          Msalabani ndiko tulikopata tabia njema, mawazo mema, mwenendo mpya, n.k

 

e.     Kututoa kwenye vifungo vya laana

Biblia inaeleza ya kwamba Yesu alipokufa pale msalabani alitutoa kwenye vifungo vya laana vilivyokuwa vimeachiliwa juu ya maisha yetu kama adhabu ya kuingia kwa dhambi duniani.

Katika historia ya Wayahudi, mtu anayetundikwa kwenye mti, jambo hilo linatafsiriwa kuwa mtu huyo ni amelaaniwa.

Kumb 21 : 22 – 23 – Aliyetundikwa kwenye mti amelaaniwa na Mungu

Wagalatia 3 : 13, 14 – Yesu akatukomboa kutoka kwenye laana

2 Wakorintho 5 : 21 – Yeye asiyejua dhambi, alimfanya kuwa dhambi kwa ajili yetu ili sisi tupate kuwa haki ya Mungu katika Yeye

Hivyo na Yesu kwa sababu yeye ni lango, (kama Adamu alivyo kuwa lango) ilimbidi afe kifo cha msalabani kwa ajili ya kuchukua laana yetu. Maana yake ni kwamba Yeye alibeba laana zetu kwa niaba yetu, ili baraka ya Mungu kupitia kwa Ibrahimu iwafikie mataifa yote kwa njia ya imani.

Kwa hiyo Yesu pale msalabani alishugulikia laana iliyokuwa juu ya kila mtu, na kwa sababu hiyo tumepokea baraka ya Mungu kupitia kwa Ibrahimu kwa njia ya kumwamini Yesu Kristo. Hivyo usipomwamini Yesu Kristo na kumpokea kwenye maisha yako huwezi ukaipata hiyo baraka.

Kwa lugha nyingine ni kuwa ndani ya msalaba wa Yesu tunapata mafanikio yetu, tunapata afya zetu, tunapata kustawi, tunapata kuongezeka na kusinga mbele zaidi n.k

Hivyo kuna kiwango cha maisha ambayo huwezi ukakifikia kama hautompokea Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako kwa sababu ndani yake ndipo tunapopokea baraka ya Ibrahimu kwa njia ya imani.

 

 

f.       Kuturejeshea mamlaka ya kiutawala tuliyopoteza

Tulipokuwa tumemuasi Mungu, tulipoteza nafasi ya kuwa watawala katika ulimwengu huu. Na sasa baada ya Yesu Kristo kufa msalabani na kutuokoa, tumerejeshwa katika nafasi ya kiutawala katika ulimwengu huu.

Yohana 1 : 12 – Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu.

1 Yohana 3 : 1 – Tazameni ni pendo la namna gani alilotupa Baba kwamba tuitwe wana wa Mungu, na ndivyo tulivyo.

Ufunuo 5 : 10 – ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu nao wanamiliki juu ya nchi

Kwa hiyo, unapookoka, moja ya jambo linalofanyika juu yako katika ulimwengu wa roho ni kukurejeshea nafasi uliokuwa umeipoteza hapo mwanzo ulipomuasi Mungu.

v  Kwa nini Mungu anakurejeshea nafasi hiyo?

Ø  Kwa sababu, Mungu ni Mfalme wa mbinguni, hivyo anavyokuja duniani ni lazima akaribishwe na mfalme wa duniani. (mfalme wa duniani ndio wewe. Ndio maana Yesu anaitwa mfalme wa wafalme – wafalme wanoongelewa hapa ni watakatifu wa Bwana)

-          Mfalme anakaribishwa na mfalme mwenzake, au raisi anakaribishwa na rais mwenzake

-          Hivyo ndivyo itifaki ilivyo katika ulimwengu wa kiroho na wa kimwili pia.

Mathayo 16 : 19 – Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni.

-          Mwenye ufunguo ndiye mwenye mamlaka.

-          Sasa huwezi ukawa na mamlaka kama huna nafasi, hivyo unapewa kwanza nafsi ndipo unapopewa na mamlaka.

-          Kwa mfano, Rais wa Tanzania, kinachompa mamlaka aliyonayo sasa ni kwa sababu anayo nafasi ya urais. Lakini akishastaafu tu kwenye hiyo nafasi basi na mamlaka yake pia yanaishia hapo. Hatoweza tena kufanya maamuzi juu ya nchi.

-          Kwa hiyo ni wazi kabisa kuwa tulipopoteza nafasi kwa sababu ya dhambi, tulipoteza pia na mamlaka yaliyotokana na nafasi hiyo.

Shetani anachokifanya ni kukupiga vita ili akuondoe kwenye nafasi uliyonayo kwa sababu anajua akikuondolea nafasi uliyonayo popote pale basi hata mamlaka pia itaondoka.

 

 

 

g.     Kuturejeshea utakatifu na kutupatanisha na Mungu

Wakolosai 1 : 19 – 22

Kipindi kile dhambi ilipoingia duniani, haikumtenga tu mwanadamu na Mungu bali ilitenga vitu vyote vilivyokuwa chini ya huyo mwanadamu na Mungu.

-          Kwa hiyo sio tu kwamba uwepo wa Mungu uliondoka kwa mwanadamu peke yake bali uwepo wa Mungu uliondoka hadi kwenye vitu vya huyo mtu kama vile ardhi.

-          Hivyo, kwa njia ya msalaba, Yesu alivipatanisha vitu vyote (ikiwa ni pamoja na mwanadamu) na nafsi yake.

-          Mwanadamu akapata kuwa mtakatifu tena kama Mungu alivyo mtakatifu.

1 Petro 1 : 15 – 16 – Kwa maana imeandikwa, mtakuwa watakatifu kwa kuwa mimi ni mtakatifu.

Hivyo, kwa njia ya msalaba tunarejeshewa utakatifu wa Kimungu na tunapatanishwa naye. Hii inamaana ya kwamba, mahusiano yanarejea tena baina yetu na Mungu wetu.

Kabla ya msalaba, watu walikuwa hawawezi kwenda mbele za Mungu moja kwa moja. Ilikuwa ni mpaka wapitie kwa kuhani mkuu na huyo kuhani mkuu ilikuwa ni lazima atoe sadaka ya kuteketezwa kwa ajili ya dhambi zake na dhambi za wale anaowaongoza ndipo aende mbele za Mungu, na tena huingia mara moja kwa mwaka.

Lakini baada ya msalaba, kila mmoja akaruhusiwa kwenda mbele za Mungu kwa njia ya Yesu Kristo. Damu ya Yesu imetupa ujasiri huo wa kukaribia patakatifu pa patakatifu.

Ebrania 10 : 19 – 20 – Kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu.

Hapo ndipo utaelewa ni kwa nini pazia la hekalu lilipasuka wakati Yesu anasulibiwa msalabani. Hiyo ilikuwa ni ishara kuwa sasa kila mtu anaruhusiwa kwenda mbele za Mungu bila kuwa na kipingamizi chochote isipokuwa kwa njia ya Damu ya Yesu Kristo tu.

Mathayo 27 : 51 – Pazia la hekalu lilipasuka vipande viwili.

Kutoka 26 : 31 – 35 – historia ya pazia la hekalu lililogawanya kati ya patakatifu, na patakatifu pa patakatifu

Kwa hiyo neema tuliyonayo sisi tunaoishi baada ya msalaba wa Yesu Kristo ni kwamba tunao ujasiri wa kumwendea Mungu moja kwa moja kwa damu ya Yesu Kristo. Hatuhitaji tuchinje kondoo wala mbuzi wala mnyama yeyote wala tulipe fedha yoyote, kwa sababu Yesu tayari alishamwaga damu yake msalabani inayoturuhusu kwenda kwa Baba

Kwa kupitia damu ya Yesu tuna uwezo wa kuwasiliana na ulimwengu wa roho. Hicho ni kitu ambacho waganga na wachawi hawawezi ila ni mpaka wachinje mnyama au ndege ili wapate damu itakayo waunganisha na ulimwengu wa roho.

 

NB: Thamani ya Yesu inatokana na msalaba. Huwezi ukamtenganisha Yesu na msalaba. Thamani ya jina la Yesu inatokana na utii wake wa kukubali kufa mauti ya msalaba

 

Hivyo msalaba, kwa kila anayemwamini Kristo ni ishara kubwa sana ya maisha yake mapya

No comments:

Post a Comment

Katika maisha yako usisikilize watu wanasema nini bali msikilize Mungu anasema nini, kwa sababu watu hawajui ni nini ambacho Mungu amekupang...