KUTOKUSAMEHE KUNAVYODHOOFISHA HALI YA KIROHO YA MTU

 Msisitizo/lengo la somo: Kukusaidia utoke kwenye madhara yanayotokana na kutokusamehe.

Somo linaeleza namna ambavyo mtu anaweza akaathirika kiroho au akadhoofika kiroho kwa sababu tu hana tabia ya kusamehe wengine wanaomkosea.

-          Inawezekana ikawa ni wazi kabisa kwamba umeokoka na wala dhambi zingine hazikusumbui yaani unajua kuziepuka na unazishinda, au ni muombaji mzuri na unaendelea kumtumikia Mungu, lakini unakwama kwenye eneo la kusamehe wanaokukosea.

-          Tabia ya kusamehe ni tabia ya Mungu, bali shetani hawezi kusamehe

-          Hivyo kutokusamehe wengine ni tabia ambayo asili yake ni Shetani.

-          Huwezi ukawa mtoto wa Mungu halafu ukawa si mtu wa kusamehe wanaokukosea.

Shetani hawezi kusamehe  ndio maana anafanya kisasi na malipizi

-          Kwa hiyo ndani yako ukiona una tabia ya kulipa kisasi – maana yake huwezi kusamehe na ndio unajitambua wazi kuwa ndani yako hayumo Roho wa Bwana bali roho ya Shetani

Mathayo 6 : 12

Biblia inasema hivi “utusamehe deni zetu kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu”

-          Huu mstari ukisoma kwa makini utagundua kuwa uzito wake upo kwenye lile neno “kama” ambapo tafsiri yake ni kwamba “tunapoomba msamaha mbele za Mungu, tunamfanya atumie kipimo kile kile tunachotumia sisi katika kuwasamehe wengine”

-          Kipimo ambacho unatumia wewe kuwasamehe wale ambao wamekukosea, ndicho kipimo hicho hicho ambacho Mungu atakitumia kukusamehe wewe makosa yako.

NB: Haijalishi huwa unaomba toba kwa muda mrefu kiasi gani, na hata kama ukataja majina yote ya Mungu lakini kama huna tabia ya kuwasamehe wale waliokukosea wewe, basi unakosa kigezo cha kusamehewa dhambi zako mbele za Mungu.

-          Hii ni kanuni katika ulimwengu wa kiroho ndani ya ufalme wa Mungu. Huwezi ukasamehewa kama wewe husamei wengine.

-          Na kitu cha ajabu ni kuwa, aliyeiweka kanuni hii ni Mungu mwenyewe.

Ni kweli kabisa kusamehe ni kazi sana na ni ngumu sana hasa pale aliyekukosea akiwa hata hajakuomba msamaha. Kibinadamu ni ngumu lakini kwa Mungu yote yanawezekana.

 

 

Tulipookoka, tuliuvua utu wa kale tukavikwa utu mpya.

Waefeso 4 : 23 – 24

Biblia inasema “na mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli

-          Nataka uyaangalie hayo maneno yaliyopigiwa mstari hapo juu.

-          Utu mpya umeumbwa kwa namna ya Mungu.

-          Kwa hiyo, hapo zamani jambo la kusamehe wengine lilikuwa ni gumu kwa sababu tulikuwa na namna ya kibinadamu (utu wa kale) ndani yetu, lakini sasa tumeokoka hivyo tumeuvaa utu mpya ambao umeumbwa kwa namna ya Mungu, kwa hiyo kusamehe halitakiwi kuwa swala gumu tena.

-          Shetani anachokifanya ni kukuletea tabia za utu wa kale wakati wewe umeuvaa utu mpya.

Utu mpya ulioumbwa kwa namna ya Mungu - maana yake utu mpya umeumbwa katika tabia ya Mungu, katika sura ya Mungu, katika utaratibu wa Mungu.

-          Hivyo yale yote ambayo ni magumu kuwezekana kibinadamu basi kwa Mungu yote yanawezekana. Ndivyo Luka 1 : 37 inavyosema.

-          Katika hayo yaliyokuwa hayawezekani kibinadamu na sasa kwa Mungu yanawezekana ni pamoja na swala la kusamehe waliotukosea.

-          Mahali pengine kwenye Biblia inasema samehe saba mara sabini- maana yake usichoke kusamehe kwa sababu hiyo ni tabia ya Mungu na sio ujinga.

-          Watu wengine wanadhani ukimsamehe aliyekukosea dunia itakuona ni mshamba. Ni kweli unaweza ukawa mshamba kwao lakini mbele za Mungu wewe ni wa thamani sana.

Kumbuka kuwa Biblia inatuambia tusiifuatishe namna ya dunia hii. Kwa hiyo tusifuate dunia inasema nini bali tufuate Bwana Yesu anasema nini.

 

KWA NINI TUNATAKIWA TUWE NA TABIA YA KUWASAMEHE WATU WALIOTUKOSEA?

Kwa nini Mungu anaweka mkazo sana sisi tuwasamehe wale waliotukosea? Kwani kuna shida gani tusipo wasamehe?

Unajua wakati mwingine unaweza ukadhani ya kwamba Mungu ni Dikteta (unadhani ya kuwa hana huruma na wewe), kwa sababu ni kama anakusisitiza uwasamehe wale waliokukosea wewe badala ya wao ndio waje kwako wakunyenyekee ili uwasamehe. Lakini ukweli ni kwamba Mungu anatupenda sana ndio maana anatuwazia mema siku zote.

Ukipita vizuri kwenye hili somo utajua ni kwa nini ni muhimu sana wewe kuwasamehe waliokukosea hata kama hawajarudi kukuomba wewe msamaha.

Tunatakiwa tusamehe kwa sababu zifuatazo:

 

1.     Ili kupata rehema au msamaha wetu kutoka kwa Mungu.

Mathayo 6 : 14 – 15 – kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi makosa yenu… msiposamehe na yeye hawasamei ninyi.

-          Anayeanza kusamehe kwanza si Mungu kwanza bali ni wewe kwanza.

-          Mungu anaangalia akiba yako ya msamaha kwa wengine ndipo anajua kama unastahili kupata msamaha au la.

-          Kusamehe wengine ni tiketi ya wewe kupata msamaha kutoka kwa Mungu. Bila hiyo tiketi huwezi kupata msamaha kutoka kwa Mungu.

-          Na kama hujapata msamaha wa Mungu maana yake huwezi pia ukashirikiana naye.

Ile “sala ya Baba yetu” inatuonyesha mambo tofauti tofauti ikiwemo vipaumbele vya ufalme wa Mungu. Sasa katika uflme wa Mungu, tunaona sheria ya msamaha ilivyo.

-          Sheria ikiwekwa mahali popote, pona yako si kuivunja sheria bali ni kuifuata sheria.

-          Sasa wewe ukiwa ni mwana wa ufalme wa mbinguni ni lazima ukatambua sheria zilizopo katika huo ufalme uliopo. Na mojawapo ya sheria ndio hiyo ya kwamba huwezi ukasamehewa kama wewe husamei wengine.

NB: Anayeanza kusamehe si Mungu kwanza bali ni wewe kwanza.

-          Wewe ndiye unayempa Mungu nafasi ya kukusamehe au kutokukusamehe.

 

2.     Ili tusiingie kwenye vifungo vya kiroho kwenye maisha yetu

Mathayo 18 : 21 – 35

-          Hii ni hadithi ya mtu mmoja aliyekuwa akifanya kazi kwa bosi wake ambaye alikuwa ni mfalme, na alifanya kosa la kupoteza kiasi kikubwa cha fedha. Bosi wake mtu huyo aliamuru huyu mtu auzwe pamoja na mke wake na watoto wake lakini huyo mtu aliomba sana msamaha naye akasamehewa. Shida ilikuja pale ambapo yeye sasa alipokutana na mtu mwingine aliyekuwa anamdai dinari, aliamua kumtesa, kitu ambacho hakikuwapendeza hata watu walioona jambo lile. Walioona wakamtaarifu Yule mfalme naye akamshika Yule mtu na kumtesa sana.

-          Biblia inasema katika mstari wa 35 kwamba “Ndivyo na Baba yangu wa mbinguni atakavyowatenda ninyi msiposamehe kwa mioyo yenu kila mtu ndugu yake”

-          Huu mstari ni mzito kupita tunavyoweza kuusoma.

-          Anachokieleza hapa ni kwamba, Mungu atawatendea wale wasiosamehe wengine vile vile kama Yule mfalme alivyomtendea Yule mtumwa wake mwovu.

 

Alimtendea nini? Alimpeleka kwa watesaji.

Kwa hiyo, Mungu naye atawesa au ataachilia mateso  (vifungo) kwenye maisha yako ambayo asili yake ni wewe kutokusamehe.

-          Maana yake hiyo ni adhabu ya Mungu kwa wale wasiokuwa na tabia ya kuwasamehe waliowakosea.

Unajua kwamba unaweza ukawa unapitia mahali fulani pagumu kwenye maisha yako, ukadhani ni Shetani ndiye aliyesababisha kumbe si Shetani bali ni adhabu ya wewe kutokusamehe wengine.

Mungu anaamua kuachilia adhabu juu yako kwa jambo ambalo kikawaida usingefikiri kama angekuadhibu.

-          Hivi ushawahi kufikiri, ni kweli kwamba huyu mtu alikuwa ana haki ya yeye kumkamata aliyekuwa anamdai dinari (tena pengine hata kumtesa ilikuwa ni haki yake). Lakini Yule mfalme alimwambia “Je haikukupasa wewe kumsamehe mjoli wako kama mimi nilivyokurehemu wewe?”

-          Maana yake ni kwamba huyu mtumwa ilimpasa yeye pia kumsamehe mjoli wake kwa sababu yeye naye alisamehewa deni lake.

 

NB: Sasa angalia jambo la ajabu kwenye hii mistari ifuatayo:

Mathayo 5 : 23 – 26 na Luka 12 : 58 – 59

Angalia yale maneno “patana na mshitaki wako mapema”

-          Kwa nini Yule aliyekukosea, Biblia inamuita mshitaki wako?

Kwa sababu, katika ulimwengu wa roho Yule aliyekukosea ndiye anayegeuka kuwa mshitaki wako. Anakuwa mshitaki wako kwa sababu hujamsamehe. Ile tu kwamba hujamsamehe, inakuwa kwako ni mashitaka.

-          Kwa hiyo, Biblia inaposema patana na mshitaki wako kwanza, hiyo ni lugha ya kiroho yenye maana ya kumsamehe.

Hivyo, ukirudi kwenye ile Mathayo 18 : 35 utaelewa kuwa Mungu anaweza akampa mtu adhabu kwa sababu ameshitakiwa mbele zake kwa kutokuwasamehe waliomkosea. Dhambi inakuwa ni kutokusamehe.  

Maisha yako yanaweza yakawa yamebanwa mahali, huwezi kujinasua hapo ukidhani ni Shetani ndiye aliyeyabana kumbe uko kifungoni. Na aliyekufunga ni Mungu mwenyewe.

-          Hakuna shida ngumu kama hiyo ya kufungwa na Mungu kwa sababu unakosa mtetezi. Hakuna wa kukuamulia.

-          Unaweza ukakemea kuanzia asubuhi mpaka jioni na bado shida yako iko pale pale.

-          Ili kutoka kwenye hiyo shida ni mpaka utambue siri hii iliyopo kwenye kusamehe wengine.

Sasa wewe mtu wa Mungu hutakiwi kuona shida katika kusamehe kwa sababu kusamehe kuna kusaidia wewe usikosane na Mungu wako.

-          Mbele za Mungu, kutokusamehe ni dhambi kama dhambi zingine.

-          Hivyo ni muhimu ukawa makini usije ukashindwa kukua kiroho kwa sababu tu umewaweka watu moyoni kwa kutokuwasamehe.

-          Anayekaa moyoni mwako ni Yesu na sio watu.

 

3.     Ili tupate amani (raha) moyoni

Unapoacha kusamehe, kinachopata shida sana ni moyo wako.

Ndio maana Mungu hawezi akaa bila kutusamehe kwa sababu kinamuumiza moyoni.

Ile Isaya 43 : 25 inasema – Mimi ndimi niyafutaye makosa yenu kwa ajili yangu mwenyewe, wala sitazikumbuka dhambi zenu.

-          Pale anaposema anatusamehe dhambi zetu kwa ajili yake, inaonyesha kuwa hatusamehewi kwa sababu tumeomba tusamehe bali ni tabia ya Mungu kutusamehe na pia hawezi kukaa bila kutusamehe.

-          Hivyo hata wewe mwanadamu ukikaa bila kusamehe ni lazima utapata shida moyoni mwako.

Mathayo 11 : 28 – 29 – ukishatua mzigo kwa Yesu utapata raha nafsini mwako au moyoni mwako.

-          Kutokusamehe ni kuweka mzigo moyoni mwako ambao utaondoa amani au raha ndani yako.

-          Na ndio maana watu wengi wameokoka lakini hawana amani au hawana furaha mioyoni mwao. Kwa sababu gani? Kwa sababu hawajui kuwasamehe watu waliowakosea.

NB: Ukikosa amani au raha moyoni mwako utakuwa umekosa kitu kikubwa sana na cha muhimu sana.

Kumbuka kwamba,

a.      Amani ndani yako ndiyo inayokupa uwe na maamuzi sahihi – Wakolosai 3 : 15

-          Ndio maana watu wengine wanakuwa ni wenye hasira za karibu na huwa hawana maamuzi sahihi kwenye mambo yao

b.      Pia, Amani ndiyo inayobeba na kuhifadhi umoja wa Roho ndani yako – Waefeso 4 : 3

-          Ukipoteza amani ndani yako ni wazi kabisa hutokuwa na ushirika mzuri na watu wengine, hata kama mnasali pamoja.

-          Mahusiano yako na watu wengine yanategmea kiwango cha amani kilichopo moyoni mwako

-          Amani ikiwepo basi mahusiano yatakuwa mazuri, lakini amani isipokuwepo na mahusiano hayatakuwa mazuri.

c.       Amani yako inaweza ikatuonyesha kiwango cha imani yako – Warumi 5 : 1

-          Biblia inatuambia kuna uhisiano kati ya amani na imani.

-          Amani ni matokeo ya imani ya kuhesabiwa haki, kwa hiyo amani ikipotea inaonyesha kwamba ni wazi kuwa imani imepotea pia.

 

Tunamuhitaji Mungu sana katika jambo hili maana si jepesi kibinadamu lakini kwa Mungu ni jepesi.

Mshirikishe Mungu katika shida yako naye atakusaidia namna ya kutoka hapo.

Hata kama huwezi kusamehe kwa sababu unaona kosa la mtu aliyekukosea ni kubwa sana, wewe nenda mbele za Mungu, jiweke wazi mbele zake, mwambie kuwa huwezi kusamehe, lakini unahitaji msaada wake. Utashangaa namna ambavyo ataachilia utulivu ndani yako na nguvu za Roho Mtakatifu zitakujilia ndani yako na hapo hapo utapokea amani moyoni na ndiyo itakusaidia kusamehe.

-          Ile ile amani ambayo inaondoka kutokana na kutokusamehe ndiyo hiyo hiyo Yesu atairudisha kwa sababu ni yeye ameuondoa mzigo wa kutokusamehe moyoni mwako.

Bwana Yesu anao uwezo wa kukusaidia kusamehe. Hata kama shida ni kubwa namna gani, wewe nenda mbele zake naye atautua mzigo wako.

No comments:

Post a Comment

Katika maisha yako usisikilize watu wanasema nini bali msikilize Mungu anasema nini, kwa sababu watu hawajui ni nini ambacho Mungu amekupang...