JIFUNZE KUONA TOFAUTI ILIYOPO KATI YA KUWA MTUMISHI WA MUNGU NA KULITUMIA JINA LA YESU

 Msisitizo: Ni kukusaidia kumtumikia Mungu kwa uaminifu huku ukitimiza unayopaswa kuyafanya.

UTANGULIZI:

Kuna tofauti kubwa sana kati ya kumtumikia Mungu na kulitumia Jina la Yesu. Kuna watu wanalitumia jina la Yesu kuombea watu, kutoa unabii, kuhubiri n.k lakini sio watumishi wa Mungu.

Somo hili linalenga kukusaidia kujua tofauti iliyopo kati ya Yule mtu ambaye ni mtumishi wa Mungu na mwingine si mtumishi wa Mungu lakini anatumia jina la Yesu akidhani ya kuwa anamtumikia Mungu.

Kumtumikia Mungu ni wito ambao mwanzilishi wake ni Mungu.

-          Wito wako ndio unaokupa kujua sababu ya kuumbwa kwako.

-          Kumtumikia Mungu ni kufanya yale mapenzi ya Mungu. (maana yake kuyajua na kuyafanya yale ambayo Mungu anataka uyafanye)

-          Kwa hiyo kama hufanyi yale anayokuagiza Bwana maana yake ni kwamba humtumikii yeye, hata kama unatumia jina lake kwenye kazi yako au huduma unayoifanya.

Luka 6 : 46 – Kwa nini mnaniita Bwana Bwana lakini hamyatendi nisemayo?

-          Hii inaonyesha wazi kabisa kwamba ili uwe ni mtumishi wa Bwana Yesu ni lazima uwe unafanya kile anachokuagiza kukifanya.

-          Kwa mfano; kuna watu wanahuduma ya kuimba, kuhubiri au kuombea wenye shida mbali mbali kwa kutaja jina la Yesu lakini hawafanyi yale ambayo Mungu anawaagiza kufanya.

Malaki 1 : 6 – “Mwana humheshimu baba yake, na mtumwa humcha bwana wake, …basi kama mimi ni bwana wenu kicho changu ki wapi”

-          Kama watumwa au watumishi hawamsikilizi bwana wao (bosi wao) wanasemaje kuwa wanamtumikia?

-          Kwa maana kumtumikia mtu ni kufanya kile anachokuagiza ukifanye.

-          Mungu hataki ufanye kile unachokijua wewe au unachokiona kuwa ni sahihi bali anataka ufanye kile anachokuagiza ukifanye. Hiyo ndio maana halisi ya kuyafanya yale yampendezayo Mungu.

NB: Kumbuka kwamba unapomtumikia Mungu, yeye ndiye anayekuambia nini cha kusema au cha kufanya unapotumika. Ni sawa na mtu anayekwenda kuhubiri halafu hapati muda wa kumuuliza Mungu nini cha kuhubiri na badala yake anakwenda kuhubiri kwa mazoea.

Biblia inasema hivi katika Mathayo 7 : 21 – 23

“si kila mtu aniambiaye Bwana Bwana atakayeingia katika ufalme wa mbinguni bali ni Yule afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile Bwana hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo? Ndipo nitawaambia dhahiri sikuwajua ninyi kamwe”

-          Hapa Bbiblia inatuambia kuwa kuna watu wanaotumia jina la Yesu katika kufanya huduma zao lakini Yesu mwenye jina hilo hawajui wao.

-          Wao wanadhani wanamtumikia Mungu lakini kumbe wanatumia tu jina la Yesu katika kufanya huduma zao lakini kiukweli hawamtumikii Mungu.

NB: Kutumia jina la Yesu bila kuwa na ushirika na Yesu huko sio kumtumikia Mungu.

-          Na kwa sababu hiyo watu wengi wanadhani  ya kwamba kule kukemea mapepo kwa kutumia jina la Yesu au kutoa unabii au kuhubiri kwa kutumia jina la Yesu ndio pekee kumtumikia Mungu, sio kweli.

-          Mungu anachotaka hapa ni wewe kuwa na ushirika naye kwanza. Kwa sababu kuwa na ushirika na Mungu ndio kutakusaidia wewe kumfahamu Mungu na kuyajua mapenzi yake ili uyafanye.

-          Ushirika na Mungu unakujulisha mapenzi ya Mungu ni nini; nini Mungu anataka wewe ufanye.

-          Kuwa na ushirika na Mungu ni jambo la muhimu sana kwa kila mtumishi kujua kabla ya kuanza utumishi wowote ule.

-          Kwa sababu kazi ya kumtumikia Mungu si ya mtumishi wa Mungu bali ni ya Mungu mwenyewe, yeye ndiye aliyekuagiza uifanye hiyo kazi, hivyo anajua nini wewe unatakiwa kukifanya.

-          Wengine wandhani utumishi ni kazi yao ndio maana wanafanya vile wanavyotaka wao na sio vile Mungu anavyotaka.

Pale Yesu aliposema “ndipo nitawaambia dhahiri sikuwajua ninyi kamwe, ondokeni kwangu ninyi mtendao maovu”

-          Neno “sikuwajua” maana yake sikuwa na uhusiano wowote na ninyi au sikuwa na ushirika wowote na ninyi.

-          Ni kweli mlitumia jina langu kuponya, na kutoa unabii na kufufua wafu lakini mimi na ninyi hatujawahi kuwa wamoja, hatujawahi kufahamiana, hatukuwa na ushirika wowote. Kwa hiyo kazi mliyoifanya nisawa na hakuna kitu.

Kwa mfano, Daktari ambaye anatibu watu katika kituo cha afya lakini hajasajiliwa na serikali.

-          Kwa hiyo serikali haimtambui japokuwa anatibu watu

-          Hata kama atakuwa anatumia dawa za serikale kutibu watu ni kweli watu watapona lakini yeye mwenyewe hatambuliki na serikali.

-          Pia ni hatari kwa afya za hao watu anaowatibu kwa sababu daktari huyo anaweza asifuate miongozo ya afya katika kutibu wagonjwa inayotolewa na serikali mara kwa mara.

Ukisoma kitabu cha Matendo 19 : 13 – 16

-          Hii ni habari ya wana saba wa mtu mmoja aliyekuwa anaitwa Skewa ambaye alikuwa ni kuhani mkuu.

-          Vijana hao walijaribu kukemea pepo kwa kutumia Jina la Yesu lakini pepo aliwaambia hivi Yesu tunamjua na Paulo naye tunamjua lakini ninyi ni akina nani?

 

MAMBO KADHAA YANAYOTOKEA KATIKA ULIMWENGU WA ROHO UNAPOKUWA NA USHIRIKA NA BWANA YESU

Mtumishi wa Mungu ni lazima uwe na ushirika na Mungu unayemtumikia. Sasa yafuatayo ni mambo ambayo yanatokea pale ambapo wewe mtumishi wa Mungu unapokuwa umetengeneza ushirika mzuri na Mungu wako.

1.     Ndani mwako unabeba sura ya Mungu

2 Korintho 4 : 3 – 4 – Kristo ni sura ya Mungu.

Yohana 14 : 7 – 11 Yesu yu ndani ya Baba na Baba yu ndani ya Yesu, hivyo aliyemuona Yesu amemuana Baba pia. Na aliyembeba Yesu amembeba Baba pia

Yohana 17 : 21 22

-          Unapompokea Bwana Yesu moyoni mwako, katika ulimwengu war oho hauonekani wewe tena bali anaonekana Yesu aliye sura ya Mungu ndani yako.

-          Wewe ulishakufa, sio wewe unayeishi tena bali ni Krsto ndiye anayeishi ndani mwako – Wagalatia 2 : 20

-          Mapepo yakikuangalia hayakuoni wewe bali yanaona sura ya Mungu ndani yako.

-          Sura ya Mungu inaonekana ndani yako kwa sababu wewe unakuwa ndani ya Yesu na Yesu anakuwa ndani yako.

-          Ndio maana utaelewa ni kwa nini Yule pepo aliwaambia wana wa Skewa kwamba Yesu tunamjua na Paulo tunamjua lakini ninyi ni wakina nani?

-          Tafsiri yake ni kwamba Yule pepo alipoangalia ndani ya mioyo ya wale wana wa Skewa hakuona sura ya Mungu ndani yao.

 

2.     Unabeba heshima ile ile aliyonayo Yesu

Yohana 17 : 22 – Nami utukufu ule ulionipa nimewapa wao …

-          Kwa lugha nyingine utukufu maana yake ni heshima au hadhi au mamlaka.

Efeso 1: 20 – 23; 2 : 6 – Yesu ameketi juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu na usultani, … akatufufua pamoja naye akatuketisha pamoja naye juu sana.

1 Yohana 3 : 1 – 2 – Ni pendo la namna gani alilotupa Baba kwamba tuitwe wana wa Mungu, … wala haijadhihirika bado tutakavyo kuwa lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye.

Katika ulimwengu wa roho, sisi tunapata kuwa na heshima ile ile aliyonayo Yesu kwa sababu tumembeba Yesu mioyoni mwetu.

Zaburi 8 : 4 – 6

Zaburi 82 : 6 – Mimi nimesema ndinyi miungu, na wana wa Aliye juu.

-          Biblia inaposema “tumeketishwa pamoja naye juu sana” maana yake mahali alipoketi Yesu ndipo na sisi tumeketi hapo hapo, kwa hiyo heshima aliyonayo Yesu ndio hiyo hiyo na sisi tuliyonayo.

NB: Kwa nini tumepata heshima kama aliyonayo Yesu? Kwa sababu katika ulimwengu wa roho kuna mamlaka tofauti tofauti za madaraka; kuna wafalme, wakuu wa anga, majeshi ya pepo wabaya n.k hivyo ili uweze kupambana nayo ni lazima na wewe uwe kwenye level au ngazi ya juu zaidi kuliko wao ndipo utaweza kuwashinda.

-          Ndio maana Biblia inasema tumeketishwa juu sana kuliko falme na mamlaka na nguvu, ikiwa inamaana ya kuwa tuko juu ya kila aina ya upinzani wowote katika ulimwengu wa roho.

-          Utumishi wowote ni vita, na ndio maana ni muhimu sana kwa mtumishi yeyote wa Mungu ajifunze kutumia nafasi yake ya kimamlaka aliyonayo rohoni ili kushinda vita katika ulimwengu wa roho.

-          Na kwa sababu hiyo unao uwezo ndani yako wa kutamka jambo nalo likatokea.

Kwa hiyo hata kama watu hawatambui thamani yako, jua ya kwamba wewe ni mtu mkuu sana na mwenye kuheshimiwa sana. Na hata mbingu zinakujua

Na pia ni muhimu sana kwa watumishi wa Mungu kujijua wao wana nafasi gani mbele za Mungu (sisi ni watoto wa Mungu aliye hai)

Nafasi tulizonazo katika ulimwengu wa roho ni heshima tunayoipata baada ya Yesu Kristo kuingia mioyoni mwetu

NB: Nafasi yoyote ile (kifalme na kikuhani) huwa ina mambo makubwa mawili

i.                    Mamlaka

-          Mamlaka ni nguvu ya kiutawala juu ya mipaka ya eneo fulani

-          Eneo letu la kiutawala ni katika ulimwengu wa roho  na wa mwili pia. Lakini eneo letu la vita ni katika ulimwengu wa roho peke yake.

2 Korintho 10 : 3 – 5

Efeso 6 : 12

 

ii.                 Majukumu / wajibu

-          Majukumu ni kazi tunazotakiwa kuzifanya kutokana na nafasi tulizonazo (nafasi ya kifalme na ya kikuhani)

-          Yeremia 1 : 4 – 10 – Yeremia anapewa kazi ya kufanya kutokana na nafasi ya kinabii aliyopewa.

-          Kila nafasi ina majukumu yake. Huwezi ukapewa nafsi isiyokuwa na majukumu.

 

3.     Mungu anakupa nafasi ya kufanya kazi pamoja naye

Yohana 15 : 14 – 15 – siwaiti tena watumwa kwa sababu mtumwa hajui atendalo bwana wake bali ninyi mmekuwa rafiki zangu.

Warumi 8 : 28 – nasi twajua ya kuwa Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema.

Ni heshima kubwa sana kufanya kazi pamoja na Mungu.

-          Si rahisi sana wakati mwingine kuelewa sentensi hiyo lakini hebu fikiria kwamba kuna wakati Mungu hatofanya jambo lolote duniani bila kukushirikisha kwanza. Hivi unajisikiaje unapopata nafasi hiyo? Amosi 3 : 7

-          Na Mungu anakushirikisha kwa sababu anajua akikuagiza uombe ni kweli utaomba au uende ukafanye jambo fulani ni kweli unakwenda kufanya.

Mungu anapokupa nafasi ya kufanya kazi pamoja naye, mambo haya yatatokea:

i.                    Yeye anapata nafasi ya kukujulisha nini cha kufanya, mahali gani, muda upi na kwa nani.

Yeremia 1 : 7 - 8

Zaburi 32 : 8

ii.                  Wewe pia unapata nafasi ya kushauriana naye nini cha kufanya  (unahojiana naye)

Isaya 43 : 26

Mathayo 16 : 19

Kama kufunga au kufungua kunaanzia duniani kwanza basi maana yake ni kuwa Mungu anakusikiliza wewe ni nini utakachoamua kukifanya naye ndipo afanye.

Mfano: Musa alikataa kuwaongoza wana wa Israel bila kuwa na Uso wa Mungu pamoja naye.

Kutoka 33 : 15

-          Musa alikuwa anajua tofauti ya kuongozwa na malaika wa Mungu, na Mungu mwenyewe.

-          Kuongozwa na Mungu sio sawa na kuongozwa na malaika. Hadhi au heshima hazifanani.

-          Iweje aanze na Mungu kisha amalize na malaika?

 

4.     Unapata kujulikana na kuaminika katika ufalme wa mbinguni.

Luka 10 : 17 – 20 – msifurahi kwa sababu pepo wanawatii bali furahini kwa kuwa majina yenu yameandikwa mbinguni.

Daniel 10 : 11 – Daniel mtu upendwaye sana.

Huku kujulikana na ufalme wa mbinguni kunatokana na uaminifu ulionao juu ya kuifanya kazi ya Mungu unayopewa. Kuna watu wanapewa kazi na Mungu za kufanya lakini wanazifanya kwa ulegevu na sio kwa uaminifu.

-          Mbingu zinarekodi kwamba mtu huyu ni mwaminifu au sio mwaminifu

-          Ni kitu kimoja wewe kumwamini Mungu lakini ni kitu kingine Mungu kukuamini wewe.

-          Hebu fikiria Mungu anakuagiza muda fulani uende ukaombe lakini wewe hauombi kwa muda ule aliokuagiza Bwana bali unakwenda kuomba kwa muda wako uliojipangia. Mbele za Mungu unaonekana sio mwaminifu.

Mwanzo 18 : 17 – 19 – Je, nimfiche Ibrahimu jambo nitakalo kulifanya… kwa maana nimemjua ya kuwa atawafundisha wazao wake juu ya njia ya Bwana.

Hesabu 12 : 1 – 7 – 8 – Yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote.

Ayubu 1 : 1 – Mtu huyo alikuwa mkamilifu na mwelekevu, ni mmoja aliyemcha Mungu na kuepukana na uovu.

Ni sawa na mfano wa mtu aliyeajiriwa serikalini.

-          Ile kwamba ameajiriwa na serikali inamaanisha kuwa serikali inamuamini ndio maana imempa ajira hiyo.

 

MSISITIZO AMBAO MUNGU ANAKUWA NAO PALE ANAPOKUPA KAZI UIFANYE (ANAPOACHILIA WITO NDANI YAKO)

Msisitizo wa Mungu katika utumishi au huduma anayokupa uifanye haupo katika umuhimu wa hiyo kazi aliyokupa bali upo katika kusikiliza na kufuata maagizo na maelekezo anayokupa.

-          Kazi au utumishi wowote ulionao ni rahisi sana kwa mtu yeyote Yule mwingine kuifanya lakini tofauti ni maelekezo.

-          Ni rahisi sana kwa watu wengi kusikiliza huduma zao zinasema nini lakini hawataki kusikiliza Mungu anasema nao nini.

-          Mfano, swala sio kuwa na kipaji cha kuimba au kuhubiri bali ni maelekezo na maagizo gani uliyopewa yanayohusu huduma yako ya kuimba au kuhubiri.

Unaweza ukahubiri kitu ambacho Mungu hajakutuma kwenda kuhubiri, Na huo ndio ugomvi mkubwa uliopo kati ya Mungu na wahubiri wengi kwa sababu wengi wanahubiri vile ambavyo Mungu hajawatuma kuhubiri. Wanahubiri wanayoyajua wao wenyewe na sio kile ambacho Mungu kawatuma kuhubiri.

Yeremia 23: 16 – 18, 22, 25 – 28 – Lakini kama wangalisimama katika baraza yangu, wangaliwasikizisha watu wangu maneno yangu.

-          Katika ulimwengu wa roho kuna eneo linaitwa baraza ya Mungu. Hapo ni mahali ambapo Mungu anakutana na watumishi wake na kuwapa maneno yake kwa ajili ya kuwapelekea watu.

-          Kwa mfano mhubiri yeyote ni lazima ujifunze kusimama barazani pa Mungu ili upokee neno kutoka kwa Bwana kwa ajili ya watu unaokwenda kuwahubiria.

NB: Usihubiri kwa sababu una kipawa cha kuhubiri bali hubiri kwa sababu Mungu amekupa neno la kuhubiri.

-          Mungu anajua kuna uhusiano uliopo kati ya Neno linalohubiriwa na hali za mioyo ya watu wanaosikia neno hilo.

-          Na ndio maana kuna watakaopokea neno hilo kama chakula cha kushibisha nafsi zao, pia kuna watakopokea neno hilo kama uponyaji wa majeraha katika miyo yao, na wapo pia watakopokea kama nguvu mpya ya kuimarisha roho zao.

-          Kwa hiyo ni muhimu kusikia kutoka kwa Bwana kwa sababu Yeye ndiye atakayekupa chakula sahihi kwa kuwa anajua watu wake wanahitaji nini na kwa muda gani.

Kwa hiyo ni vyema ukajua kuwa kuna watu wanaweza wakapona kwa neno unalokwenda kuwahubiria au wanaweza wakapotea kwa neno hilo hilo unalokwenda kuwahubiria.

Yeremia 23 : 1 – 2, 16 – 17

-          Hebu angalia, hilo ni neno linalotoka madhabahuni lakini linawaharibu watu badala ya kuwajenga na kuwasaidia.

-          Unaweza ukaenda mahali inawezekana ikawa ni kwenye mkutano fulani au kanisa fulani na ukasikiliza mahubiri lakini baada ya yale mahubiri kumalizika unaanza kujisikia huzuni au unahisi kukosa amani moyoni mwako. Roho mtakatifu ndani mwako anapiga kelele kukuambia kuwa kuna chakula kimeingia moyoni mwako lakini si kizuri kwa afya ya roho yako.

-          Ni sawa na gari inayotumia mafuta ya petrol halafu wewe ukaenda kuweka mafuta ya diesel. Haitawaka bali itapata shida.

Hivyo ni hatari sana kuitii huduma uliyonayo kuliko kumtii Mungu aliyekupa hiyo huduma.

-          Unapoweka huduma moyoni basi utaisikiliza zaidi huduma uliyonayo badala ya kumsikiliza Mungu . ni rahisi sana kufuata akili zako badala ya kufuata maelekezo unayopewa na Mungu.

-          Yesu ndiye anayekaa moyoni na sio huduma.

-          Ukimweka Yesu moyoni, utamsikiliza yeye zaidi. Lakini ukiweka huduma moyoni basi utaisikiliza zaidi huduma

Ufunuo 3 : 20 – Yesu anakaa moyoni

Yohana 14 : 23 - Yesu na Baba watakuja kufanya makao ndani ya mtu

Zaburi 119 : 11 – moyoni nimeliweka neno ambaye ni Yesu

Yohana 1 : 1 - Yesu ni Neno ambalo linatakiwa likae moyoni

 

Yesu anapokuja kukaa ndani yako, haji peke yake bali anakuja pamoja na Baba kwa sababu Yesu yu ndani ya Baba na Baba yu ndani ya Yesu.

 

Baadhi ya mifano ya watu walioweka huduma na utumishiwao moyoni badala ya kumweka Mungu moyoni mwao; na kwa sababu hiyo wakasikiliza sana huduma zao badala ya kusikiliza maelekezo ya Mungu.

a.      Utoaji wa sadaka wa Kaini

Kutoa sadaka ni utumishi. Unaweza ukaielekeza sadaka yako madhabahuni au mahali pale ambapo Bwana atakutuma uipeleke

Mwanzo 4 : 3 – 5

Waebrania 11 : 4

-          Biblia inaeleza wazi kuwa hawa ndugu wawili walikuja kutoa sadaka mbele za Bwana.

-          Huku kwenye kitabu cha Mwanzo hatuonyeshwi wazo la kutoa sadaka lilitoka wapi lakini kitabu cha Waebrania kinatuambia “kwa imani” – maana yake wazo hilo lilitoka kwa Mungu kwa kuwasemesha mioyoni mwao.

Kufuatana na Warumi 10 : 17 – Biblia inasema “basi imani chanzo chake ni kusikia, na kusikia huja kwa neno la Kristo”

-          Kwa hiyo lile neno “kwa imani” maana yake ni kwamba Kaini na Habili wote walisikia neno la Bwana juu ya agizo la kwenda kutoa sadaka.

NB: Agizo lilikuwa moja lakini maelekezo yalikuwa ni tofauti.

-          Wote Kaini na Habili walifuata agizo la kutoa sadaka bali kilicho watofautisha ni utekelezaji wa maelekezo binafsi waliyopewa.

-          Shida haipo kwenye agizo bali shida ipo kwenye kufuata maelekezo

-          Unaweza ukapatia kufuata agizo la kwenda kuhubiri lakini ukakosea kwenye maelekezo ya nini cha kuhubiri na wapi pa kuhubiri na kwa nani unatakiwa ukamhubirie.

-          Mfano: mtume Petro na Paulo hawa wote ni mitume na wameitwa kuwa mitume wa Yesu Kristo bali tofauti yao ni kwamba Petro kapewa injili ya waliotahiriwa (kwa Wayahudi) na Paulo amepewa injili ya wasiotahiriwa (kwa wamataifa.)

-          Hapo ndipo pia utakapojua kuwa Kaini hakukataliwa kwa sababu ya kutofuata agizo bali kwa kutofuata maelekezo.

 

b.      Mfalme Sauli alipotoa sadaka ikakataliwa.

1 Samweli 15 : 1 – 3, 9, 10 – 11, 14 – 15 – 23

Habari hii inaeleza namna ambavyo mfalme Sauli alipewa agizo na maelekezo ya kulipa kisasi cha Bwana juu ya Waamaleki.

-          Agizo lilikuwa ni kwenda kuwapiga Waamaleki, na maelekezo yalikuwa ni kuwaangamiza kabisa bila kuacha hai chochote binadamu wala mnyama.

-          Lakini cha ajabu Sauli alichopatia ni kufanya agizo aliloambiwa lakini akakosea kwenye maelekezo aliyopewa. Kwani aliacha hai baadhi ya mifugo akinia kwamba aje kumtolea Mungu sadaka.

-          Mungu akamkasirikia kwa sababu ya kutofuata maelekezo aliyompa japokuwa alitimiza agizo la kwenda kuwapiga Waamaleki.

NB: Kwenye kila utumishi ambao Mungu amewapa watu wake kuna kuwa na agizo na maelekezo

-          Agizo linaweza likawa ni la pamoja lakini maelekzo yakawa ni kibinafsi

-          Wote mnaweza mkawa ni wahubiri wa injili mmepewa agizo la kuhubiri lakini maelekezo ya kuhubiri yakwa ni tofauti, kama vili ilivyokuwa kwa Mtume Petro yeye alipewa injili ya waliotahiriwa na Paulo alipewa injili ya wasiotahiriwa japo wote wawili walikuwa ni mitume.

-          Kwa hiyo usijaribu kuiga huduma ya mwenzako anatumiaje.

Hapo ndipo utakapoelewa vizuri nini maana yake alipowaambia wale watu kuwa sikuwajua ninyi. (Mathatyo 7 : 21)

 

 

 

 

 

JINA LA YESU

Jina la Yesu ni jina la Mungu Baba mwenyewe

Tuanze kuangalia pale Yesu alipokuwa anazaliwa.

Luka 1 : 31 – 33

“Tazama utachukua mimba na kuzaa motto mwanamume, na jina lake utamwita Yesu”

Mathayo 1 : 20 – 21

“Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto akisema, Yusufu mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariam mkeo, maana mimba yake ni kwa uwezo wa Roho Mt, naye atazaa mwana nawe utamwita jina lake Yesu”

Je, umeshawahi kujiuliza kwa nini Yusufu na Mariam waliambiwa ya kuwa mtoto huyo atakayezaliwa jina lake wamwite Yesu? Je, hili jina lilitokea wapi? Kungetokea nini kama mtoto huyo asingepewa jina Yesu? Hebu tafakari juu ya haya maswali yatakusaidia kuchochea kiu ya kutaka kujua siri iliyopo katika jina hili la ajabu

Sababu kubwa mbili za Yesu kupewa jina hili ni hizi zifuatazo:

1.      Ni mrithi

Waebrania 1 : 1 – 4

Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu, Yeye kwa kuwa ni mng'ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu; amefanyika bora kupita malaika, kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao.

-          Yesu ni mrithi wa vitu vyote kutoka kwa Baba. Mojawapo ya vitu alivyovirithi ni jina la Baba yake ambalo ni Yesu.

-          Kumbuka kuwa huwezi ukarithi kitu ambacho ni cha kwako unarithi kitu kisichokuwa cha kwako, na pia huwezi ukarithi jina lako bali unarithi jina lisilo la kwako.

-          Kwa hiyo Biblia inaposema “kwa kadiri jina alilolirithi” maana yake jina hilo halikuwa la kwake bali la Yule aliyemrithisha ambaye ni Mungu Baba.

-          Na kwa sababu Mwana wa Mungu alikuwa ni mrithi wa yote basi ilibidi pia arithi na jina pia.

-          Hivyo Biblia inapotuambia kuwa Baba alimpa Mwana jina lake maana yake ni kwamba jina hili hapo awali lilikuwa ni jina la kwake Baba mpaka pale alipoamua kumpa Mwana jina hilo kama sehemu ya urithi kwa kuwa Mwana alikuwa ni mrithi wa yote.

Yohana 5 : 43 – “Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu, wala ninyi hamnipokei; mwingine akija kwa jina lake mwenyewe, mtampokea huyo.

-          Yesu mwenyewe anasema kwa sababu amekuja kwa jina la Baba yake ndio maana hatumpokei bali angekuja kwa jina lake mwenyewe tungempokea.

Hapo ndipo utakapolewa kwa nini anasema jina hili ni bora kuliko majina yote mbinguni, duniani, na chini ya nchi- kuzimu (Ebrania 1 : 4 & Wafilipi 2 : 9 – 10)

Kwa hiyo Mungu Baba amempa Mwana jina hilo ili ajulikane kwa hilo. Hapa utaelewa pale Yesu alipokua akituombea kwa Baba yake katika kitabu cha Yohana 17 : 6, 11, 12, 26 - “….Jina lako nimewadhihirishia watu wale ulionipa katika ulimwengu…Wala mimi simo tena ulimwenguni, lakini hawa wamo ulimwenguni, nami naja kwako. Baba mtakatifu, Kwa jina lako ulilonipa uwalinde hawa, ili wawe na umoja kama sisi tulivyo. Nilipokuwapo pamoja nao, Mimi naliwalinda Kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza….Nami naliwajulisha jina lako, tena nitawajulisha hilo….” 

-          Kwa hiyo Mungu katika agano jipya anajifunua katika jina la Yesu.

 

2.      Ni mtii 

Wafilipi 2 : 9 – 10

 “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba”.

Hii sentensi inayosema, “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina”; inatuonyesha ya kuwa ‘Kwa hiyo tena Mungu’ aliamua kumpa mtoto wake jina lipitalo kila jina; jina la Yesu kwa kuwa mtoto wake alifanya jambo Fulani lililompendeza.

-          Jambo hili ni lipi? Ni UTII – alikuwa mtii hata mauti; naam, mauti ya msalaba

 

Imeandikwa hivi katika Wafilipi 2:5-8

 Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu; ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu; tena, alipoonekana ana umbo kama mwanadamu, alijinyenyekeza akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba 

-          Yesu alikuwa ni mtii kwa kila alichokuwa anaagizwa kufanya na Baba yake

-          Na ndio maana Yesu alikuwa anaujasiri wa kusema “mimi siyatafuti mapenzi yangu mwenyewe bali mapenzi ya Yule aliyenipeleka” Yohana 5 : 30

Na kwa sababu pia alikuwa anayafanya yale yampendezayo Baba yake, basin a Baba pia alikuwa pamoja na Mwana kila mahali kwa sababu ya jina lake.

-           Yohana 8 : 28 – 29 “…na yakuwa sifanyi neno lolote kwa nafsi yangu, ila kama Baba alivyonifundisha ndivyo ninenavyo. Naye aiyenipeleka yu pamoja nami, hakuniacha peke yangu kwa sababu nafanya siku zote yale yampendezayo”

-          Kwa hiyo Mungu Baba yupo pamoja na Bwana Yesu kwa sababu ya jina lake.

NB: Jina la Yesu limebeba uwepo wa Yesu. Hivyo jina la Yesu lina mamlaka kuliko majina yote ya mbinguni, duniani na chini ya ardhi-kuzimu.

Na sisi pia tumepewa jina la Yesu Kristo

Warumi 8 : 16 – 17 “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama tu watoto basi tu warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo; naam tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye”

-          Kufuatana na Yohana 1 : 12 – sisi tunafanyika kuwa wana wa Mungu pale tunapompokea Yesu Kristo maishani mwetu. Na kwa sababu hiyo na sisi pia ni warithi sawa na Yesu Kristo tukirithi yote kwa Baba yetu aliye mbinguni.

-          Na kitu kimoja wapo tunachorithi ni jina la Yesu ambalo ni jina la Mungu Baba.

-          Kwa hiyo uwepo wa Mungu unakuwa ndani yetu kwa sababu ya jina la Yesu.

 

MUNGU ANAJULIKANA MAHALI KWA KUPITIA JINA LAKE

Mungu anaweza akajitambulisha kwa watu au akajifunua kwa watu kutokana na Jina lake. Kuna watu ambao walimfahamu Mungu na akajifunua kwao kwa namna ya tofauti na wengine walimvyomfahamu.

Mathayo 6 : 9 “Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje”

-          Angalia yale maneno yanayosema “Jina lako litukuzwe” maana yake jina lako lijulikane au lifahamike au litambulike.

-          Mungu akitaka ajulikane mahali huwa anajifunua katika jina lake kwa sababu jina lake limebeba uwepo wake na pia jina lake limebeba kazi yake.

Yohana 17 : 6 “Jina lako nimewadhihirishia” maana yake wamelijua jina lako, wamelifahamu

Mungu anapenda kutukuzwa.

-          Sasa anatukuzwaje?

-          Kwa kupitia jina lake. Jina lake linapotukuzwa yeye ndiye anatukuzwa. Kwa sababu jina lake linamaanisha uwepo wake.

Angalia kile kipindi ambacho Mungu alimtuma Musa kuwatoa wana wa Israel katika nchi ya utumwa:

            Kutoka 3 : 13 : 13 – 14 – Musa aliuliza, je, nikienda niwaambie huyo Mungu aliyekutuma kwetu anaitwa nani? Mungu akamjibu

-          Unaweza ukajiuliza kama mimi nilivyojiuliza, kwamba kwa nini Waisrael walitaka kujua jina la Mungu aliyemtuma Musa wakati alishawaambia kuwa Yeye ni Mungu wa baba zao Ibrahimu, Isaka na Yakobo?

-          Wana wa Israel walikuwa wanajua kwamba Mungu anaposhuka mahali na akajidhihirisha kwao basi jina lake linatambulisha kazi yake, hivyo walijua kweli ni Mungu wa baba zao na alijifunua kwao lakini baba zao hao hawakuwa utumwani kama wao walivyokuwa utumwani kwa hiyo alivyojifunua kwa baba zao ni tofauti atakavyojifunua kwao. Ndio maana walitaka kumjua jina lake kwa sababu walikuwa wanajua jina lake litawajulisha Mungu anayewasaidia atajifunua kwao kwa namna gani.

 

Pia ukisoma Kutoka 6 : 2 – 3 – Biblia inaeleza kwamba Mungu hakujulikana kwa akina Ibrahimu, Isaka na Yakobo kwa Jina la YEHOVA bali alijulikana kwa jina la Mungu Mwenyezi.

-          Hivyo hiyo inatuonyesha wazi kabisa kwamba Mungu alivyojifunua kwa wana wa Israel ambao walikuwa utumwani ni tofauti na alivyojifunua kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo, ndio maana akasema kwao sikujulikana kwa jina la Yehova bali kwa jina la Mungu Mwenyezi.

Mwanzo 17 : 1         Ibrahimu anamfahamu Mungu Mwenyezi

Mwanzo 28 : 1 – 3   Isaka anamfahamu Mungu Mwenyezi

Mwanzo 35 : 11       Yakobo anamfahamu Mungu Mwenyezi

NB: Mungu anataka ajulikane duniani ndio maana anataka jina lake lijulikane na litukuzwe kwa sababu jina lake ndio jina kuu kuliko majina yote na ndio limebeba uwepo wake.

Mahali ambapo kuna jina lake basi ndio penye uwepo wake:

 

Kumb 12 : 10 – 11 – 14

Biblia inasema kuwa mahali atakapopachagua Bwana ili aliketishe jina lake hapo ndipo mtakapomtolea Mungu sadaka zenu na ndipo ambapo mtakapoabudu. Kwa hiyo ni wazi kabisa kwamba mahali penye jina la Yesu basi pana uwepo wa Yesu.

Wakati mwingine tutapata neema ya kujifunza zaidi kuhusu Jina la Yesu.

MAMLAKA NA UWEZA WA JINA LA YESU

Kwa kupitia jina la Yesu;

ü  Matendo 4 : 12 – tunaokolewa

ü  Marko 16 : 17 – 18 – tunatoa pepo (mfano: Matendo 16 : 16- 18), tunasema kwa lugha mpya, tunaweka mikono yetu juu ya wagonjwa nao watapata afya na hata tukinywa vitu vya kufisha havitatudhuru.

Kwa hiyo ukitaka kulitumia jina la Yesu Kristo kihalali na uweze kuona uwezo na mamlaka yake ni muhimu kwanza, uwe mwana wa Mungu kwa kumpokea Kristo moyonimwakokama Bwana na mwokozi wako; pili, uwe mtii ukifuata maagizo ya neno la Mungu katika Roho Mtakatifu.

Sasa unaweza ukajiuliza swali hili;

Kama mtu anayemwamini Mungu ndiye anayeweza kulitumia jina la Yesu kwa usahihi, kwa nini basi kuna watu watalitumia jina hili la Yesu kutoa unabii, kutoa pepo n.k angali sio watumishi wa Mungu?

Jibu:

Jibu la swali hili lipo katika mfano huu: Serikali ina utaratibu wa kusajili madaktari wanaotibu magonjwa ya binadamu (medical doctors), sasa kuna watu ambao wako huku mitaani na inawezekana wamefungua maduka ya dawa na wanatibu watu bila ya kuwa na leseni zinazowaruhusu wao kutibu. Lakini kiukweli ukienda pale kupata msada wa kitabibu utaupata hata kama hana leseni ya udaktari.

-          Sasa hapa elewa kwamba hata kama daktari hana leseni ya kutibu lakini akakupatia dawa sahihi ya kuponya ugonjwa wako ni wazi kuwa utapona, kwa sababu kinachokuponyesha ni dawa na sio leseni yake. Hivyo ndivyo na watu wanaotumia jina la Yesu lakini wao wenyewe hawajulikani na huyo Yesu mwenyewe.

 

Ni maombi yangu kuwa Mungu akakujulishe tumaini la wito wako katika Kristo Yesu kama ulivyo ili umtumikie kwa furaha huku ukumtukuza Yesu moyoni mwako.

No comments:

Post a Comment

Katika maisha yako usisikilize watu wanasema nini bali msikilize Mungu anasema nini, kwa sababu watu hawajui ni nini ambacho Mungu amekupang...