JIFUNZE KUTUMIA MAOMBI KAMA NJIA MOJAWAPO YA KUULETA UFALME WA MUNGU MAHALI ULIPO

 Msisitizo: Ni kukusaidia wewe muombaji kujua namna ya kupanga kwanza vipaumbele vya Mungu kwenye ajenda zako za maombi kabla ya vipaumbele vyako.

Mara nyingi waombaji huwa tunapenda kuombea sana mambo yanayotuhusu sisi wenyewe na kwa muda au kiasi kidogo sana ndio tunakumbuka kuombea mambo ya nchi au mkoa au kanisa au familia n.k.

Muda mwingi muombaj anaoutumia kuomba huwa anautumia kumueleza Mungu shida zake na haja zake lakini hatumii muda mwingi kuombea makusudi na mipango ya ufalme wa Mungu mahali alipo.

Mstari unaotuongoza ni Ezekiel 22 : 29 – 31

“… nami nikatafuta mtu miongoni mwao atakayelitengeneza boma na kusimama mbele zangu mahali palipobomoka, kwa ajili ya nchi nisije nikaiharibu, lakini sikuona mtu. …”

Ukitazama kwa makini lile neno “nami” sio mwanzo wa sentensi bali linaonyesha mwendelezo wa jambo lililokuwa linazungumziwa hapo nyuma.

-          Kwenye huo mstari wa 29, Biblia inazungumzia habari za dhuluma, uonevu na kutokutoa haki kwa maskini, hali ambazo zinatokea katika nchi. Ndipo akasema “name nikatafuta mtu”.

Huu mstari hauwezi ukauelewa vizuri kama hujaelewa kwanza nini maana ya ufalme wa Mungu na aina ya waombaji ambao Mungu anawahitaji juu ya kuombea ajenda za ufalme wake.

 

MAMBO YA MUHIMU YA KUFAHAMU KUHUSU WAOMBAJI:

1.      Mungu ndiye anayetufanya kuwa waombaji.

Ufunuo 5 : 9 – 10

-          Angalia lile neno “ukawafanya kuwa makuhani

-          Kwa lugha nyepesi, kuhani ni muombaji.

-          Kuwa muombaji si jambo unalolitaka au unalolipata mwanadamu kwa sababu umestahili hapana bali ni heshima au nafasi ambayo Mungu anakupa kwa makusudi yake. Waebrania 5 : 1 – 4.

-          Tafsiri yake ni kwamba, unapopewa nafasi ya kuomba si kwa sababu wamekosekana watu wa kuomba au kwa sababu wewe unasali kwenye kanisa lenye ratiba nyingi za maombi, bali ni Mungu mwenyewe kakupa hiyo nafasi ili uitumie kwa ajili ya makusudi yake. Na katika hayo makusudi yake ndipo atakapokuteremshia ajenda zake za kuombea.

-          Ule mstari wa kwanza unasema “kuhani amewekwa kwa ajili ya wanadamu katika mambo yamhusuyo Mungu”. Maana yake ni kwamba ni lazima ndani yako Mungu ataachilia msukumo wa kuombea mambo ambayo si mahitaji yako bali ni vipaumbele vya ufalme wake.

Biblia inasema, damu ya Yesu ilimnunulia Mungu watu wa kila kabila, na lugha na jamaa na taifa, ikiwa inamaanisha kwamba Mungu ameweka waombaji katika ngazi ya familia (jamaa), kwenye kila lugha, kila kabila, na hata kila taifa.

-          Kote huko Mungu ameweka waombaji watakaoombea mambo ya ufalme wa Mungu zaidi ya kuombea mahitaji yao binafsi.

-          Msukumo uliopo ndani ya waombaji wa aina hii ni kuhakikisha wanaona ufalme wa Mungu unadhihirika mahali ambapo wamewekwa kupaombea.

-          Kama mtu amewekwa kuombea familia yake, basi hatoomba tu juu ya mafanikio yake binfsi bali ataomba juu ya familia yake imjue Mungu wa kweli na iishi na kufanikiwa ndani ya huyo Mungu wanayemtumikia. Vivyo hivyo na kwa waombaji wa kanisa au kabila au taifa, ajenda yao kubwa ni kwanza Mungu ajulikane mahali walipo.

Kwa hiyo ni muhimu kujua kwamba Mungu aliwatengeneza waombaji kwa makusudi yake. Na amewaweka mahali mahali ili kuombea ufalme wa Mungu kujulikana mahali wanapopaombea, kama ni kanisani basi ufalme wa Mungu udhihirike, au kama ni kwenye familia basi ufalme wa Mungu udhihirike na kama ni kwenye taifa basi Mungu ajulikane kwenye hilo taifa.

2.      Misingi au vipaumbele vya ufalme wa Mungu

Ufalme wa Mungu una misingi yake ambayo ni muhimu kuifahamu.

Ukisoma kile kitabu cha Mathayo 6 : 33 Biblia inasema “Bali utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake na hayo yote mtazidishiwa”

Mahali popote utakapo kuwepo ni lazima utangulize ajenda ya ufalme wa Mungu kwanza kabla ya kutanguliza maslahi yako binafsi.

-          Hebu fikiria pale unapokuwa unatafuta kazi (yoyote ile), wazo la kwanza kukujia akilini mwako ni kiasi cha mshahara unachotaka kulipwa. Lakini ukweli ni kwamba kabla ya kupata mshahara unatakiwa kutoa huduma kwanza ndipo upewe mshahara wako.

-          Je ulishawahi kuifikiria hiyo huduma utakayokuwa unaitoa ukishapata hiyo kazi kama inaendana na vipaumbele vya ufalme wa Mungu?

-          Hapo ndipo utakapojua kwamba si kila kazi utakayotakiwa kuiomba au kuifanya hata kama watakulipa mshahara mzuri.

Mungu anachotaka kwanza si kumueleza mahitaji yetu bali ni kuona tukiomba mapenzi yake yatimizwe kwanza. Sisi tunayo mipango yetu juu ya maisha yetu lakini pia Mungu anayo mipango yake juu ya hayo hayo maisha yetu. Kwa hiyo cha Mungu ndiyo kifanyike kwanza.

 

Na pia ukisoma Warumi 14 : 17 inasema:

“Maana ufalme wa Mungu si kula na kunywa, bali ni haki, na amani, na furaha katika Roho Mtakatifu”

Hii ndio misingi ya ufalme wa Mungu (HAKI, AMANI, NA FURAHA)

v  Haki

Ni kuyajua mapenzi ya Mungu kwako, na mapenzi yako kwa Mungu.

Nini Mungu anataka atende kwako, na nini unataka Mungu akutendee.

v  Amani

Amani maana yake ni kutokuwa karibu na hofu.

Yeremia 30 : 5 – Maana Bwana asema hivi, tumesikia sauti ya tetemeko na ya hofu wala si ya amani.

Kinyume cha amani ni hofu. Amani ikiondoka basi hofu inatawala.

Isaya 54 : 14 – Utathibitika katika haki, mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa, na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia.

Kuwa na amani ni kuwa mbali na maonezi.

Usipoijua haki yako, shetani bado atakuonea tu na utabaki kuita ni mapito ya Bwana au ni majaribu ya kuniongezea imani.

v  Furaha

Jambo lolote ambalo halikuletei furaha ndani ya moyo wako bali linakuletea huzuni ya kukudhoofisha au kukukatisha tamaa basi msingi wa jambo hilo sio ufalme wa Mungu.

Kinyume cha furaha ni huzuni.

Wafilipi 4 : 4 – (7) Biblia inasema “Na amani ya Mungu ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu.”

-          Lile neno kuhifadhi maana yake ni kulinda. Kwa hiyo, amani ya Mungu ina kazi moja wapo ya kuulinda moyo wako, isiingie huzuni itakayoondoa tumaini uliloliweka juu ya Bwana katika mazingira unayopitia.

-          Hapo mwanzoni mwa hii mistari anaonyesha kuwa mtu anaombea mambo yake na haja zake zinajulikana kwa Mungu, na inaonekana kabisa mtu huyu pia anaombea ajenda za ufalme wa Mungu ndio maana Mungu anaituma amani yake ili ihifadhi moyo wake na nia yake asije akakata tamaa kabla Mungu hajamjibu maombi yake.

-          Ile amani inayotunza moyo wako ndiyo inayokupa kufurahi katika Bwana siku zote kwa sababu unaendelea kumwamini na kumtegemea Mungu.

Kwa hiyo, hivyo ndiyo misingi au viashiria vya ufalme wa Mungu mahali Fulani, na Mungu mwenyewe huwa anavifuatilia.

 

Mpaka hapa sasa ndipo utaelewa kwa urahisi kidogo ule mstari wa Ezekiel 22 : 29 – 31

-          Pale ambapo Mungu anatafuta mtu atakayeomba toba na rehema juu ya mahali ambapo ufalme wake haupo.

-          Ule mstari wa 29 unaelezea kuhusu mambo ya dhuluma na kutokutendeka kwa haki juu ya nchi. Tafsiri yake ni kwamba misingi ya ufalme wa Mungu (haki, amani na furaha) haipo katika hilo eneo ndio maana anatafuta mtu wa kuomba.

-          Muombaji wa namna hii huwa anaomba toba na rehema ili Mungu arudishe ufalme wake ulioondoka kwa sababu ya dhambi.

-          Kumbuka: kinachoondoa ufalme wa Mungu mahali ni dhambi. Kwa hiyo muombaji anaomba toba ili dhambi iondoke na isiwe na nguvu tena bali ufalme wa Mungu ujengwe na uwe na nguvu mahali hapo.

Waombaji wa ajenda za ufalme wa Mungu ndani yao watakuwa na msukumo wa kuombea juu ya haki kutendeka, kuwa na amani na furaha.

-          Wewe ambaye umepewa mzigo wa kuombea taifa utashangaa kila unapoona dhuluma kwenye nchi au maonezi yoyote yale utasikia msukumo wa kuomba toba juu ya nchi na kuachilia tena ufalme wa Mungu kuja tena mahali pale.

-          Na hata yule anayeombea familia au kanisa ni wazi kwamba utakapoona haki hakuna, wala furaha na amani hakuna mahali ulipo, kuna maonezi ya maskini na kunyimwa haki zao, basi utajua kuwa ni dhambi imeingia ikaharibu mahali hapo na ndio maana ufalme wa Mungu umeondoka.

NB: Unachotakiwa kufanya ni kuomba toba na rehema juu ya mahali hapo ili Mungu aachilie msamaha wake na asipaharibu.

 

Hivyo basi utakapoisoma tena hiyo Ezekieli 22 : 29 – 31 utaona mambo yafuatayo:

i.                    Mungu anakumbuka rehema katikati ya ghadhabu

-          Anaposema “nami nikatafuta mtu …. Nisije nikaiharibu nchi”. Hii inaonyesha wazi kuwa Mungu wetu kabla hajaadhibu mahali popote huwa kwanza anakumbuka rehema juu ya watu wake hata kama wamekosa.

-          Mwanzo 18 : 23 – 26 – Kabla Mungu hajaangamiza miji ya Sodoma na Gomora alitafuta mtu kwanza wa kuomba toba juu yao ili asiwaangamize. Japo muombaji (Ibrahimu) hakufikia kiasi cha maombi kilichohitajika kuiponya ile miji.

 

ii.                  Yapo mahusiano katika ulimwengu wa kiroho kati ya Mungu na mahali Fulani (taifa, kabila, familia, kanisa n.k)

-          Katika ulimwengu wa kiroho, familia yako, kabila lako, taifa lako n.k ni baadhi ya maeneo ambayo Mungu anaweka uhusiano wake na hayo maeneo kwa kuusimamisha ufalme wake mahali hapo.

-          Na kama ikitokea dhambi ikaingia mahali hapo basi inaharibu mahusiano hayo ya Mungu na hilo eneo.

-          Kwa hiyo mahali hapo pakitawaliwa na dhambi basi panaitwa “mahali palipobomoka”, maana yake panahitaji matengenezo, laa sivyo, adhabu ya Mungu itashuka mahali hapo.

-          Hivyo Mungu anaweza akaipiga familia au kabila, au taifa kwa sababu mahusiano yameharibika na ufalme wake umeondoka kwa hiyo hakuna tena watu wanaotenda haki, hofu na huzuni ndiyo vilivyotawala.

 

iii.                Mungu anahitaji angalau mtu mmoja tu ili aiponye nchi

-          Nami nikatafuta mtu… hajasema kwamba akatafuta watu bali akatafuta mtu.

-          Maana yake ni kwamba hata kama wote wametenda dhambi kwenye familia au kwenye nchi na hasira ya Mungu ikawa juu ya eneo hilo basi pakitokea tu mtu mmoja mwenye haki akasimama kwa ajili ya kuomba rehema kwa Mungu ili Mungu asipaangamize mahali hapo, ujue kwamba Mungu hatopaangamiza mahali hapo na ataparehemu kabisa kwa ajili ya huyo aliyeomba.

-          Yeremia 5 : 1 – muombaji mmoja mwenye haki anayo nafasi ya kuzuia ghadhabu ya Mungu isiwake juu ya mahali au nchi au familia iliyomkosea Mungu.

-          Mithali 14 : 34 –“ haki huinua taifa bali dhambi ni aibu ya watu wowote”.

-          Mwenye haki mmoja anayo nafasi ya kuokoa taifa zima kwa hiyo haki yake.

Hivyo mpendwa usijidharau ukajiona huna thamani yoyote mbele za watu kwa kuwa mbele za Mungu wewe ni wa thamani sana.

-          Mungu amekuweka kwenye hiyo familia kwa makusudi yake, ndio maana inawezekana kwamba wewe ndio mtu pekee uliyeokoka kwenye ukoo mzima. Wala kisikusumbue, kwa sababu kwa kupitia wewe Mungu anakwenda kuokoa ukoo mzima au familia nzima.

-          Unapokuwa unaombea kwa mfano familia yako ni sawa na kumwambia Mungu kwamba asiadhibu familia yako kutokana na dhambi zilizopo kwenye hiyo familia, bali aiokoe kutoka kwenye maangamizi.

 

Mungu anatafuta angalau mtu mmoja tu ili aiponye nchi, au kanisa, au familia n.k.

-          Wa kuiponya familia yako ni wewe muombaji.

-          Wa kuiponya nchi yako au kanisa lako ni wewe muombaji.

-          Madhara yoyote yanapotokea juu ya nchi au familia au kabila au kanisa, wa kwanza kuulizwa ni wanamaombi waliowekwa kuyaombea hayo maeneo.

Mungu haangalii wingi wa watu wanoomba juu ya mahali fulani bali anaangalia watu wanoombea vipaombele vya ufalme wake.

-          Kanisa linaweza likawa na waombaji wengi kwa idadi lakini wakawa ni waombaji wasiokuwa na tija kwa taifa kwa sababu ya kutumia muda wao mwingi katika kuombea shida zao binafsi badala ya kuombea ajenda za ufalme wa Mungu.

-          Mungu amekuweka hapo ulipo kwa makusudi kabisa ili kuujenga ufalme wake kwa kupitia maombi yako. Hivyo usijidharau hata kidogo.

 

 

No comments:

Post a Comment

Katika maisha yako usisikilize watu wanasema nini bali msikilize Mungu anasema nini, kwa sababu watu hawajui ni nini ambacho Mungu amekupang...